Rwanda yatangaza tena kumsaka Kayumba Nyamwasa

Muktasari:
Serikali ya Rwanda imetaka Afrika Kusini kumkamata Nyamwasa na kuzuia mali zake zote zilizopo nchini humo
Kigali, Rwanda. Serikali ya Rwanda imetoa hati kadhaa za kimataifa kufuatia mashambulizi ya hivi karibuni kusini mwa nchi hiyo ikiwasaka watu mbalimbali akiwemo Jenerali Kayumba Nyamwasa.
Wengine wanaosakwa ni wafuasi wa kundi la P5 ambalo ni ni jukwaa la vyama vya siasa vya upinzani nchini humo ambavyo vinatuhumiwa kuanzisha uasi Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo dhidi ya Serikali ya Rwanda.
Hata hivyo jukwaa hilo limekuwa likikanusha madai hayo.
Jenerali Nyamwasa, mkuu wa zamani wa majeshi ya Rwanda amekuwa akiishi Afrika Kusini ambapo Rwanda inataka akamatwe na mali zake zote zizuiwe.
Julai mwaka jana, vyama hivyo viliomba kuandaliwa kwa mazungumzo ya kisiasa na Rais Paul Kagame, ombi ambalo mpaka sasa halijapata jibu.
Nyamwasa alikuwa mtu wa karibu na Rais Kagame ambaye kwa sasa anaishi nchini Afrika Kusini chini ya ulinzi mkali wa Idara ya Usalama nchini humo baada ya jaribio la kutaka kumuuua mwaka 2010.
Kiongozi huyo wa chama cha upinzani cha RNC pamoja na vyama vingine wanatuhumiwa na utawala wa Kagame kuanzisha uasi Mashariki mwa DRC katika eneo la Fizi na Uvira.
Hati hizo zimetolewa katika kipindi hiki kisichokuwa na uhusiano mzuri kati ya Rwanda na DRC na kati ya Rwanda na Afrika Kusini.