Samia: Kuna vyombo vya habari mlivifungia, vifungulieni

Samia: Kuna vyombo vya habari mlivifungia, vifungulieni

Muktasari:

  • Rais wa Tanzania,  Samia Suluhu Hassan ameitaka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kuvifungulia vyombo vya habari vilivyofungiwa na kuagiza wahusika kutotumia ubabe kuvidhibiti.

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania,  Samia Suluhu Hassan ameitaka Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kuvifungulia vyombo vya habari vilivyofungiwa na kuagiza wahusika kutotumia ubabe kuvidhibiti.

Akizungumza leo Jumanne Aprili 6, 2021 Ikulu jijini Dar es Salaam wakati wa kuwaapisha makatibu wakuu na naibu makatibu wakuu amesema wizara ihakikishe vyombo vya habari vinafuata sheria na miongozo iliyoweka

“Nasikia kuna vyombo vya habari mlivifungia, vifungulieni na vifuate sheria tusiwape mdomo kwamba tunaminya uhuru wa kuzungumza. Tusifungie kibabe, wafungulieni na kuhakikisha wanafuata kanuni na miongozo ya Serikali.”

“Watakapofanya makosa adhabu zitolewe kulingana na sheria inavyoelekeza, viacheni vifanye kazi yao isionekane wanazuiwa kuongea,” amesema Samia.

Rais pia amesisitiza wizara hiyo ambayo inahusika pia na michezo, sanaa na  utamaduni kusimamia haki za wasanii na wanamichezo kuhakikisha kundi hilo wananufaika na kazi zao.

Kwa takribani miaka mitano sasa vyombo mbalimbali vya habari nchini hasa magazeti vilisitishiwa leseni za uchapaji na usambazaji kwa muda na vingine kutakiwa kuomba upya leseni.

Kati ya magazeti yaliyofungiwa na hadi sasa hayajarejea kwenye uchapishaji ni gazeti la Tanzania Daima.