Serikali yatoa ufafanuzi wanaolipishwa wakijifungua

Mbunge wa Temeke (CCM), Dorothy Kilave akiuliza swali bungeni leo Februari 7, 2023 .Picha na Said Khamis

Muktasari:

  • Suala la wanawake wanaojifungua kulipishwa gharama za upasuaji limetinga bungeni, ambapo Mbunge wa Temeke (CCM), Dorothy Kilave amehoji mpango wa Serikali wa kukabiliana na changamoto hiyo.

Dodoma. Mbunge wa Temeke (CCM), Dorothy Kilave amesema wanawake wanaojifungua kwa njia ya upasuaji wamekuwa wakilipishwa Sh100, 000 katika vituo vya afya wakati katika Hospitali ya Wilaya ya Temeke wamekuwa wakilipa Sh200, 000.

 Akiuliza swali la nyiongeza, leo Jumanne Februari 7, 2023 Dorothy amehoji Serikali inampango gani wa kupunguza kabisa gharama hizo.

Pia amehoji Serikali inampango gani wa kutoa vifaa vya kujifungulia kwa wanawake ili kuondoa gharama za kununua vifaa hivyo ikiwemo pamba.

Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Afya, Dk Godwin Mollel amesema suala ni la kisera kuwa wajawazito na watoto chini ya miaka mitano hawatakiwi kulipishwa matibabu.

Amewaomba wakuu wa wilaya na mikoa kushirikiana na Wizara ya Afya kusimamia suala hilo.

Dk Godwin amesema ametembea katika vituo vya afya na hospitali za wilaya mkoani Dar es Salaam na kubaini kuwa vituo vya afya vinapata wagonjwa wengi kuliko hata hospitali za wilaya.

“Wakati mwingine mgawo wanaoupata MSD (Bohari ya Dawa Nchini) wanaishiwa mapema kulikoni idadi ya watu na hata zaidi ya watoto 160,000 wanazaliwa maana yake mgawo wa MSD ni mdogo,”amesema.

Amesema watahakikisha kuwa mgawo wa dawa pamona na vifaa unaendana idadi ya watu bila kuangalia kama ni kituo cha afya ama hospitali.