TMA yatoa tahadhari ya mafuriko, mvua kubwa ikitarajiwa mikoa sita nchini
What you need to know:
Mvua kubwa zinatarajiwa kunyesha kwa siku mbili katika mikoa sita ambazo zinaweza kuleta athari katika mikoa hiyo
Dar es Salaam. Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesema mvua kubwa zinatarajiwa kunyesha kwa siku mbili katika mikoa sita na kuleta athari katika mikoa hiyo.
Mikoa inayotarajiwa kunyesha mvua hizo ni Iringa, Njombe, Lindi Mtwara, Ruvuma na Morogoro.
Taarifa ya TMA iliyotolewa leo Jumamosi Desemba 26, 2020 imesema mvua hizo zinatarajiwa kunyesha juu ya wastani kuanzia leo hadi Desemba 27, 2020.
Inasema zinaweza kusababisha mafuriko na barabara kutopitika na baadhi ya makazi ya watu kuzungukwa na maji na kuwataka wananchi kuchukua tahadhali.
Pia, TMA imetoaa tahadhali ya kuwepo kwa mawimbi makubwa yanayofikia ukubwa wa mita 2.0 na upepo unaokwenda kasi kilometa 40 kwa saa utakaosababisha kuathiri shughuli za uvuvi, usafiri baharini na upatikanaji wa samaki.
Imesema upepo huo unatarajiwa kuanza Desemba 28, 2020 maeneo ya Pwani ya bahari ya Hindi katika mikoa ya Lindi, Mtwara, Dar es Salaam, Pwani, Tanga, Mafia, Unguja na Pemba.
TMA imewashauri watumiaji wa bahari ya Hindi wachukue tahadhali na hatua stahiki huku wakiendelea kufuatilia hali hiyo a watatoa mrejeo kila itakapobidi.