Turkish Airlines yarejesha safari zake Tanzania
Muktasari:
- Shirika la Ndege la Turkish Airlines la nchini Uturuki ambalo lilisitisha safari zake nchini 2020 kutokana na mlipuko wa ugonjwa wa Uviko 19 limetangaza kurejesha na safari zake June 2022 .
Hai. Shirika la Ndege la Turkish Airlines la nchini Uturuki ambalo lilisitisha safari zake nchini 2020 kutokana na mlipuko wa ugonjwa wa Uviko 19 limetangaza kurejesha na safari zake June 2022 .
Hayo yamesemwa na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA), Christine Mwakatobe wakati aakieleza uongozi wa kiwanja hicho cha ndege (KADCO) ulivyopokea tuzo ya umahiri wa rasilimali watu katika uwakilishi wa wanawake kwenye ngazi ya Menejimenti.
Amesema shirika hilo litakuwa linafanya safari zake mara nne kwa wiki kupitia uwanja wa KIA.
"Menejimenti ya KADCO kwa kushirikiana na wadau mwaka huu wa fedha ambao tupo sasa tumefanikiwa pakubwa sana, Mwezi Oktoba mwaka jana tulipokea Shirika la ndege la Ederecy kutoka Zurich kuja Kilimanjaro ambalo linakuja mara mbili kwa wiki, June 4 mwaka huu tutapokea tena shirika la ndege jipya la Eurowings discover ambalo litakuwa linatoka Frankfurt Mombassa kuja Kilimanjaro.
"June 20, 2022 Shirika la Ndege la Uturuki, Turkish Airlines ambalo lilisitisha safari zake mwezi Machi, 2020 wakati wa ugonjwa wa Uviko 19 litaanza kurudi tena rasmi mara nne kwa wiki,"amesema Mwakatobe
Amesema kurejea kwa mashirika hayo hapa nchini ni mafanikio katika uwanja huo wa ndege wa KIA ambapo amesema ni wakati mwafaka hasa katika uzinduzi wa Royal Tour ambao umefanywa na Rais Samia Suluhu Hassan katika kuutangaza utalii duniani.