Viongozi Chadema wahudhuria mahakamani kesi ya wabunge

Muktasari:

Wabunge wawili na wafuasi 36 wa Chadema wanakabiliwa na mashtaka manane.

Morogoro. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe na mjumbe wa kamati kuu ya chama hicho, Frederick Sumaye, wamehudhuria katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Morogoro ambako uamuzi wa dhamana ya wanachama wa chama hicho utatolewa.

Wengine waliofika mahakamani ni mbunge wa Tarime Vijijini, John Heche na wa Viti Maalumu, Devota Minja. 

Wabunge Susan Kiwanga na Peter Lijualikali wamefikishwa katika Mahakama hiyo leo Jumanne Desemba 5,2017 kusikiliza uamuzi wa dhamana yao pamoja washtakiwa wengine 36.

Kesi hiyo ipo mbele ya hakimu Ivan Msack. Ulinzi umeimarishwa ndani na nje ya Mahakama, huku barabara zote zinazoelekea mahakamani zikiwa zimefungwa. 

Washtakiwa wanatetewa na mawakili Peter Kibatala, Ignas Punge, Fredrick Kiwelo na Bartholomew Tarimo. 

Upande wa mashtaka unawakilishwa na mawakili wa Serikali, Edga Bantulaki na Sunday Hyera. 

Washtakiwa wanakabiliwa na mashtaka manane likiwemo la kuchoma moto ofisi ya Kata ya Sofi iliyopo wilayani Malinyi.