Wabunge wataka Bunge lisimame kujadili panya rodi, Spika asema...

Muktasari:

Spika wa Bunge la Tanzania, Dk Tulia Ackson ameiagiza Serikali kufuatilia matukio ya uhalifu yanayofanywa na makundi ya vijana maarufu Panya road katika mikoa mbalimbali ikiwemo jijini Dar es Salaam.

Dodoma. Vifo vinavyotokana na matukio ya uvamizi wa vijana maarufu panya rodi, vimewaibua wabunge nchini Tanzania wakitaka Bunge liahirishwe ili kujadili jambo hilo.

Hata hivyo, Spika wa Bunge, Dk Tulia Akson amezima hoja hiyo akiiagiza Serikali kushughulikia jambo hilo kwa haraka na dharura.

Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Bahati Ndingo ametoa hoja hiyo kwa Bunge akitaka shughuli zingine ziahirishwe kwa ajili ya kujadili suala hilo.

Hoja kama ya Bahati ilikuwa imeombwa na Mbunge wa Segerea (CCM), Bona Kamoli (CCM) ambaye naye alipendekeza shughuli za Bunge simame ili wajadili hali hiyo.

Katika hoja yake, Ndingo amesema hali ni mbaya katika maeneo mengi akitaja mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma, Mara na maeneo mengi kwamba usalama wa watu na mali zao umekuwa mdogo.

"Mheshimiwa Spika, hali ni mbaya katika maeneo mengi na jana tulisikia huko Dar es Salaam, lakini jirani yangu huyu Dk Chaya (Pius mbunge wa Manyoni Mashariki) jirani yake diwani amevamiwa na hao panya road, usalama wa watu na mali zao sasa ni mdogo, naomba tujadili," amesema Ndingo.

Akijibu mwongozo huo, Spika Dk Tulia Akson amekiri kumekuwa na shida katika maeneo mengi na hivyo usalama wa watu na mali zao umekuwa mashakani.

Hata hivyo, Dk Tulia amesema kanuni ya 55 haitoi nafasi ya wabunge kujadili jambo hilo isipokuwa akaagiza Serikali kulifanyia kazi kwa haraka na udharura ili bunge lipewe taarifa.