Wachungaji waomba kukumbukwa mapambo ya Uviko-19

Muktasari:

  • Wachungaji wa madhehebu mbalimbali mkoani Mbeya wameiomba Serikali kuwapa motisha kwa ushiriki wao katika mapambano ya ugonjwa wa Uviko-19.

  

Mbeya. Wachungaji wa madhehebu mbalimbali mkoani Mbeya wameiomba Serikali kuwapa motisha kwa ushiriki wao katika mapambano ya ugonjwa wa Uviko-19.

Akizungumza leo Oktoba 13 kwenye kikao cha tathimini ya chanjo ya Uviko 19 cha kamati ya msingi mkoa kikichoitishwa na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera, Mchungaji wa Kanisa la Pentekoste, Aibross John amesema wana makundi makubwa wanayoyahamasisha.

Mchungaji John amesema kuwa wachungaji wamekuwa wakibeba mzigo mkubwa wa kuhamasisha na kutoa elimu kwa waumini hususani kwa kundi la vijana kujitokeza kupata chanjo ya Uviko-19 kwa awamu ya tatu na kufanikisha mkoa kumaliza dozi zikizoletwa mkoani hapa.

"Serikali kupitia Wizara ya afya, tunaomba ituone kwa kutupatia motisha, kwani elimu inayotolewa na viongozi wa dini imeleta matokeo mazuri ya kuongezeka kwa kundi kubwa la waumini kujitoa kuchanja chanjo ya uviko 19 kupitia makundi ya vijana makanisani.

"Mkuu wa Mkoa tuko pamoja na wewe tunaomba magari ya matangazo kutengeneza mazingira ya kuwafikia watu wengi kwenye mikusanyiko ili ya watu ili kuwarahisishia watoa huduma," amesema.

Kwa upande wake Shekhe Ibrahim Bombo amesema kuwa changamoto kubwa  ya baadhi ya jamii kuwa nyuma kuchanja ni baadhi ya  viongozi wa dini kuwalaghai waumini kwa madai kuwa  imefika katika misikiti na makanisani kwa maslai ya watu wachache.



Naye Katibu wa Machifu Mkoa wa Mbeya, Michael Yilanga ameomba wataama wa afya kutoa tahadhari kwa vijana kutokana na wengi wao kitumia vilevi hivyo kuokoa maisha yao

Akizungumza katika mkutano huo, Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera amewataka watoa huduma wa chanjo ya Uviko-19 kuzingatia staha za mavazi pindi wanapokwenda kutoa elimu na kuchanja waumini wa madhehebu kulingana na imani za dini.

"Watoa huduma angalieni maeneo mnayokwenda kutoa chanjo ya uviko 19 kwa kuvaa nguo nzuri ili kutoleta madhara ya kihisia na kwamba Mkoa wa Mbeya ulipokea chanjo 50,000 ambazo zote zimekwisha," amesema.

Homera amesema kuwa ushirikiano mkubwa wa viongozi wa dini zote umechochea idadi kubwa ya waumini kuchanja chanjo ya awali na sasa wanasubiri chanjo mpya ambayo itaingia wakati wowote kuanzia sasa," amesema.