Wanajeshi SADC wafa DRC kwa kombora, rambirambi zatumwa kwa Tanzania, Afrika Kusini
Muktasari:
Ni wale waliotumwa na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) kwenda nchini DRC kwa ajili ya kulinda amani
Dar es Salaam. Wanajeshi watatu wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) waliopo kwenye Operesheni katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (SAMIDRC) wamepoteza maisha na wengine watatu kujeruhiwa mashariki mwa DRC.
Wanajeshi watatu waliojeruhiwa ni kutoka Tanzania, taarifa ya SADC iliyotolewa kwa umma leo Aprili 8, 2024 imebainisha hayo ikisema, tukio hilo la kusitisha limesababishwa na kombora lililoangukia karibu na kambi ya wanajeshi hao.
“Tukio hili la kusikitisha lilitokea baada ya kombora kuangukia karibu na kambi waliyokuwa wakiishi. SAMIDRC inasikitika kutangaza kifo cha mwanajeshi wa Afrika Kusini aliyefariki wakati akipatiwa matibabu kutokana na changamoto za kiafya katika Hospitali ya Goma, DRC,” imeandikwa kwenye taarifa hiyo.
“Wanajeshi hao walitumwa nchini DRC chini ya uangalizi wa SADC kama sehemu ya kukabiliana na hali mbaya ya usalama Mashariki mwa DRC,”
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, “familia ya SADC inatoa salamu za rambirambi kwa familia wapendwa hao Serikali ya Jamhuri ya Afrika Kusini na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa msiba huo na wakati huohuo, tunawatakia ahueni ya haraka askari watatu waliojeruhiwa.”
“SAMIDRC itaendelea kujikita katika kutekeleza majukumu yake kulingana na kanuni ya ulinzi wa pamoja na hatua za pamoja zilizoainishwa katika Mkataba wa Ulinzi wa Pamoja wa SADC (2003).
Ikumbukwe Januari mwaka huu, Jeshi la Kongo lilitangaza kuanzisha operesheni ya pamoja na wanajeshi wa kikosi cha Jumuiya ya nchi za SADC dhidi ya waasi wa M23 Mashariki mwa Kongo.
Kikosi hicho cha SAMIDRC kinajumuisha wanajeshi kutoka Malawi, Afrika Kusini na Tanzania.