Wananchi 24,000 kunufaika na mradi wa maji Rombo
Muktasari:
- Mradi wa maji wa Njoro II uliogharimu Sh4.9 bilioni umeanza kutekelezwa mkoani Kilimanjaro utakaomaliza changamoto ya uhaba wa maji kwa zaidi ya wananchi 24,000 katika Tarafa za Tarekea, Usseri, Mashati na Wilaya ya Rombo
Rombo. Mradi wa maji wa Njoro II uliogharimu Sh4.9 bilioni umeanza kutekelezwa mkoani Kilimanjaro utakaomaliza changamoto ya uhaba wa maji kwa zaidi ya wananchi 24,000 katika Tarafa za Tarekea, Usseri, Mashati na Wilaya ya Rombo
Mradi huo umeanza kutekelezwa Aprili 2022 ambapo utakuwa na uwezo wa kuzalisha mita za ujazo 1728 kwa siku.
Hayo yamesemwa na Ofisa Huduma kwa wateja wa Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Rombo (Rombowassa), Selestine Mtenga wakati akijibu changamoto za wananchi kuhusu tatizo la maji Katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kata ya Mamsera wilayani humo.
"Katika kutatua changamoto ya maji Wilaya ya Rombo ipo miradi ambayo inatekelezwa na Serikali mfano mradi wa Njoro II ambapo chanzo chake cha maji kipo msitu wa Rongai. Mradi huu umeshatekelezwa kwa awamu ya kwanza na ukikamilika utaondoa tatizo la maji katika Tarafa 3” amesema
Akizungumzia miradi huo Waziri wa Elimu, Profesa Adolf Mkenda amesema Serikali imetengea zaidi ya Sh10 bilioni kumaliza tatizo la maji wilayani humo.
"Kwa mwaka mmoja wilaya hii imepata Sh10 bilioni kwa ajili ya kukabiliana na changamoto ya maji, tunamshukuru Rais Samia Suluhu Hassan pamoja na Waziri wa maji, Jumaa Aweso kwa kuona uhitaji huu mkubwa wa maji katika wilaya hii," amesema Profesa Mkenda ambaye pia ni Mbunge wa Rombo
Naye Mkazi wa Kata ya Mamsera, Joseph Msai amesema mgao wa maji wilayani humo umekuwa ni changamoto kubwa ambapo wakati mwingine maji hutoka baada ya wiki moja au mbili