Wapenzi wafariki wakiwa wamelala chumbani Njombe

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Njombe, Hamisi Issah

Muktasari:

  • Watu wawili wamefariki dunia mkoani Njombe baada ya kuingia na jiko la mkaa katika chumba cha kulala kwa ajili ya kupunguza baridi.

Njombe. Watu wawili wamefariki dunia mkoani Njombe baada ya kuingia na jiko la mkaa katika chumba cha kulala kwa ajili ya kupunguza baridi.

Hayo yalibainishwa leo Jumatano Julai 21, 2021 na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Njombe, Hamisi Issah wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika makao makuu ya jeshi hilo mkoani hapa.

Alisema marehemu hao waliokutwa na umauti walifahamika kwa majina ya Benitho Mbatha (23) mpiga debe wa mjini Njombe na Jazila Said ambaye kabila ni Mndendeule (27) mkazi wa Namtumbo mkoani Ruvuma.

“Baada ya kufariki hakuna mtu ambaye aligundua kama kuna watu wamefariki, tukio hili limetokea tarehe 17 mwezi wa saba majira ya saa tano na nusu huko mtaa nwa National Housing kata ya Njombe mjini wakiwa wamelala kwenye chumba kimoja,”alisema Issah.

Alisema sababu ya kifo chao inaonyesha wakati wakiwa hai waliweka moto wa mkaa kwa ajili ya kujihifadhi na baridi ambapo mtindo huo umekuwa ukitumika na watu wengi mkoani Njombe.

Aidha Kamanda Issa alitoa wito kwa wananchi wa Mkoa wa Njombe kutumia njia nyingine kujikinga na baridi na si kuota moto kama ambavyo wengi wamekuwa wakifanya kwa kwani kufanya hivyo ni hatari kwa maisha yao.

“Niwaombe wananchi wewe unaona chumba chako ni kidogo na unatumia mkaa ndani hiyo ni hatari nyingine na huko lilikotokea tukio chumba ni kidogo na kina dirisha moja na dogo sana. Acheni kulala na jiko ndani ya nyumba sasa hivi ni hatari tafuteni nguo nzito nzito za kuzuia baridi lakini sio moto wa mkaa,”alisema Issah.

Alisema tukio hilo ni la tatu kutokea mkoani Njombe kutokana na tukio jingine kumkuta dada mkazi wa Songea aliyekuwa mhudumu wa baa moja mjini Njombe kufariki ndani kwa jiko la mkaa huku mwingine akifariki wilayani Wanging’ombe kwa jiko la mkaa.

Mmiliki wa nyumba aliyokuwa akiishiri marehemu Benitho Mbata, Amani Samsoni alisema yeye alikuwa wa kwanza kushuhudia tukio hilo baada ya kwenda kumtembelea marehemu na kuwaona wote wawili wakiwa wamefariki

“Lakini bado mimi nilifuatilia kwa majirani wanasema yule mwanamke alikuwa anaelekea Madaba,alikosa nauli na huyu kijana kwa kuwa yupo pale kwenye magari akamwambia njoo upumzike kwanza na kesho nitakusaidia nauli ya kukufikisha kwenu kwa hiyo hiki kitu kinahuzunisha sana”alisema Samson

Kwa upande wao majirani akiwemo Winfrida Msalilwa alisema “Marehemu huwa anapenda sana kuja hapa na alikuja pia akachukua moto na akachukua chipsi mayai akasema nina mgeni wangu huko ndani lakini siku baada ya siku tukashangaa haonekani mpaka tulipoona wanakuja polisi" alisema Winifridal.

 Alisema sio vizuri kwenda kulala sehemu usioijua kwa mfano hapo huyo mwanaume angefariki halafu angebaki mwanamke tayari angekuwa na kesi ya kujibu”alisema Msalilwa.