Watu tisa wafariki dunia ajali ya basi, 30 wajeruhiwa
Muktasari:
- Watu tisa wamefariki dunia na wengine zaidi ya 30 wamejeruhiwa baada ya basi linalofanya safari zake kati ya Babati Mkoa wa Manyara na Dar es Salaam kupinduka.
Dodoma. Watu tisa wamefariki dunia na wengine zaidi ya 30 wamejeruhiwa baada ya basi la Emigrace linalofanya safari zake kati ya Babati Mkoa wa Manyara na Dar es Salaam kupinduka.
Ajali hiyo imetokea leo Jumamosi Oktoba 2, 2021 katika mteremko wa milima ya Kolo Wilaya ya Kondoa mkoani Dodoma.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk Besta Magoma amesema miili ya watu hao imehifadhiwa Hospitali ya Wilaya ya Kondoa.
“Bado tunaendelea na uokoaji, idadi kamili ya majeruhi tutaijua baada ya kumaliza. Sasa hivi tunaendelea kuwapa rufaa majeruhi kwenda katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma,”amesema.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Dodoma, Onesmo Lyanga hakupatikana kulizungumzia tukio hilo.