Wawili wanusurika ajalini

wawili wanusurika ajalini

Muktasari:

  • Watu wawili wamenusurika kifo baada ya gari aina ya  Hiace waliyokuwa wamepanda kutoka Kigoma mjini kwenda Wilaya ya Uvinza kuteketea kwa moto.

Kigoma. Watu wawili wamenusurika kifo baada ya gari aina ya  Hiace waliyokuwa wamepanda kutoka Kigoma mjini kwenda Wilaya ya Uvinza kuteketea kwa moto.

Ajali hiyo imetokea leo Alhamisi Juni 10, 2021 saa 11 jioni katika eneo la Mikamba wilayani Kigoma huku kondakta na dereva wakipata majeraha.

Wakisimulia ajali hiyo ilivyotokea wakati wakipelekwa hospitali ya rufaa ya Maweni dereva wa gari hilo, Ezra Yohana amesema wakiwa safarini gari hilo lilipata hitilafu na kuamua kushusha abiria ili walipeleke gereji.

Amesema wakiwa njiani gari hilo lilipata hitilafu ya umeme na kuanza kuwaka moto,” nililazimika kutokea dirishani ili nijiokoe baada ya milango kugoma kufunguka.”

Kondakta wa gari hilo,  Hamisi Nzingo amesema awali gari hilo halikuwa na tatizo lolote.

Kaimu mganga mfawidhi wa hospitali ya Maweni, Frank Sudai amesema waliwapokea majeruhi wawili na kwamba dereva hali yake si nzuri kwa kuwa ameungua zaidi ya mwenzake ambaye ameruhusiwa.

Kamanda wa polisi Mkoa wa Kigoma, James Manyama amesema hana taarifa kuhusu tukio hilo.