Waziri Ummy; Wawajibisheni ila msiwapeleke mahabusu

Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu akizungumza na watumishi wa afya wa Mkoa wa Simiyu (hawapo pichani) wakati wa ziara ya ukaguzi wa utoaji wa huduma za afya na upatikanaji wa vifaa tiba mkoani humo, kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Dk Yahya Nawanda. Picha na Samirah Yusuph

Muktasari:

Amesema licha ya makosa ya kitaaluma ya watumishi wa kada hiyo kutafutiwa suluhu katika mabaraza yao ya kitaaluma inabidi wao wajitambue na kuwajibika bila kushurutishwa.

Bariadi. Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amewaagiza wakuu wa mikoa na wilaya nchini kutoona haya kuwawajibisha watumishi wa afya wanapokwenda kinyume na muongozo wa utumishi wa kada hiyo.

Agizo hilo amelitoa leo Jumatatu Julai 10, 2023 wakati wa ziara yake ya kukagua utoaji wa huduma za afya na upatikanaji na vifaa tiba katika hospitali za Mkoa wa Simiyu akiwataka kutowapeleka mahabusu.

“Ukishakuwa ni mtu wa afya unaongozwa na weledi, tumeona upuuzi na vitu vya ovyo vinavyofanywa na watumishi idara ya afya na ninafurahi wamekuwa wakichukuliwa hatua ninadhani inabidi tuongeze kidogo nguvu ya kuwabana ili kuongeza uwajibikaji mie nitaendelea kuwatetea,”amesema Ummy

Amesema licha ya makosa ya kitaaluma ya watumishi wa kada hiyo kutafutiwa suluhu katika mabaraza yao ya kitaaluma inabidi wao wajitambue na kuwajibika bila kushurutishwa.

“Mzingatie maadili na viapo vyenu vya kazi, ninaendelea kusisitiza kuzingatia weledi hilo ni kwaajili yenu ili kuwaokoa na maambikizi wakati wa kazi,”amesema

Akitoa taarifa ya afya ya mkoa huo, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Boniphace Marwa ameiomba Serikali kuwa na mikakati endelevu ya kuwajengea uwezo watumishi walio katika vituo vya ngazi ya msingi ambayo haina wagonjwa wengi.

“Kutokakana na kuboreshwa kwa miundombinu ya afya ili kuweza kutoa huduma bora tunaomba mafunzo ya kuwajengea uwezo kutokana na na upanuzi wa huduma nyeti kama vile ICU, EMD na huduma za watoto wachanga,”amesema Dk Marwa

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Dk Yahya Nawanda amesema mkoa huo umeimarika katika utoaji wa huduma za afya na hivyo huna uhitaji mkubwa wa madaktari bingwa hasa wa magonjwa ya damu.