Zaidi ya askari 24,000 wapandishwa vyeo tangu Rais Samia aingie madarakani

Zaidi ya askari 24,000 wapandishwa vyeo tangu Rais Samia aingie madarakani

Muktasari:

  • Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania, Simon Sirro amesema kwa kipindi kifupi tangu Rais Samia Suluhu Hassan alichoshika uongozi ametoa kibali cha kupandishwa vyeo maaskari 24, 850.


Dar es Salaam. Mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania, Simon Sirro amesema kwa kipindi kifupi tangu Rais Samia Suluhu Hassan alichoshika uongozi ametoa kibali cha kupandishwa vyeo maaskari 24, 850.

Sirro ameeleza kuwa haijawahi kutokea wakati mmoja idadi hiyo ya askari kupandishwa vyeo.

IGP amezungumza hayo leo Jumatano Agosti 25, 2021 katika Kikao Kazi cha Maafisa Wakuu Waandamizi wa Jeshi hilo, amesema kwa kipindi kifupi tangu Rais kuingia madarakani amefanya makubwa ambayo hayakuwahi kufanywa kwenye historia ya Jeshi hilo.

Ameeleza jambo lingine ni kutoa kibali cha ajira mbadala kwa askari 3,103 akieleza kuwa kwa miaka mitano walipata kibali cha ajira za askari wapya 812.

Jambo la tatu ni kutoa zaidi ya Sh40.2 bilioni kwa ajili ya kulipa malimbikizo ya madeni ya wazabuni.

Kutoa Sh12.3 bilioni kwa ajili ya kulipa malimbikizo ya madeni ya stahiki za askari na Sh2.7 bilioni kwa ajili ya kulipa malimbikizo ya wastaafu.

“Kwa hiyo ile kelele ya wastaafu imekwisha sasa na kubaki kuwa historia. Nikushukuru sana mheshimiwa Rais kwa hatua hii,”

Lingine lililofanyika ni ununuzi wa helkopta mpya ya polisi aina ya Airbus huku Sirro akibainisha kuwa mara ya mwisho jeshi hilo kununuliwa helkopta ilikuwa mwaka 1984.