Watanzania asilimia 6.5 hawana vyoo kabisa

Muktasari:

  • Matokeo ya haya yote, ni maradhi kwa maelfu ya watoto ambao hupoteza mai-sha kila mwaka kwa sababu ya maradhi yanayoweza kuzuilika ikiwamo kuhara na kipindupindu.Vyoo bora pamoja na kusafisha mikono ingeokoa nusu ya vifo hivi. Kwani hata wale waliona vyoo, suala la kunawa mikono kwa sabuni halizingatiwi kabisa wakati wa kutoka chooni na kabla ya kuanza kula chakula.Utafiti unaonyesha kutokutumia vyoo na kunasababisha uwapo wa nusu ya watoto waliodumaa kwenye jamii.

Watanzania wengi hutumia vyoo visivyokuwa bora na hawaoshi mikono kwa maji safi na sabuni.Inaelezwa zaidi ya nusu yao hutumia vyoo vilivyo chini ya kiwango na moja ya kumi sawa na asilimia 6.5 hawatumii vyoo kabisa.

Matokeo ya haya yote, ni maradhi kwa maelfu ya watoto ambao hupoteza mai-sha kila mwaka kwa sababu ya maradhi yanayoweza kuzuilika ikiwamo kuhara na kipindupindu.Vyoo bora pamoja na kusafisha mikono ingeokoa nusu ya vifo hivi. Kwani hata wale waliona vyoo, suala la kunawa mikono kwa sabuni halizingatiwi kabisa wakati wa kutoka chooni na kabla ya kuanza kula chakula.Utafiti unaonyesha kutokutumia vyoo na kunasababisha uwapo wa nusu ya watoto waliodumaa kwenye jamii.

Tanzania inaelezewa kuwa na kiwango cha juu cha watoto wenye udumavu dun-iani, imeelezwa watoto milioni 2.7 wame-dumaa. Hawa ni watoto ambao wapo kwenye hatari ya kuambukizwa maradhi na watakuwa na uwezo mdogo kiakili na matokeo mabaya ya kielimu, kadiri wana-vyokuwa. Wanapokuwa watu wazima, wanakuwa na uwezo mdogo kwa asilimia 20 chini ya wale ambao hawakudumaa.“Maendeleo yetu ya kiuchumi yanarudi nyuma.

Kutokuthamini usafi wa mazin-gira kunatugharimu zaidi ya Sh340 bilioni ikiwa ni katika muda uliopotea, afya isiy-okuwa bora na maendeleo duni,” anasema Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jin-sia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu.Anasema hiyo ni sawa na asilimia moja ya pato la taifa ambayo thamani yake inal-ingana na thamani ya umeme unaotumika nchini kote. Ummy anasema nchi kwa sasa inajikita katika kurekebisha hali hiyo mwaka hadi mwaka na ifikapo 2025, inakusudia kufikia uchumi wa kati au zaidi.“Wito wangu kwa wadau wa maendeleo, tunataka tuwe na kampeni moja nchini badala ya kuweka rasilimali fedha zetu sehemu mbalimbali, badala yake tuun-ganishe nguvu, tufanye kampeni moja ya usafi wa mazingira na mabadiliko ya tabia nchini,” anasema.Anatoa maagizo kwa maofisa afya kuz-ingatia hali za usafi wa mazingira kwani Tanzania haiwezi kuwa nchi yenye uchumi wa kati ikiwa usafi hautazingatiwa.“Awamu ya tano tunazungumzia kuokoa fedha za Serikali na kuzielekeza kwa jamii kwenye mambo yanayogusa wananchi moja kwa moja. “Huu ni uchambuzi wa Benki ya Dunia, tunapoteza Sh340 bilioni kila mwaka kuto-kana na kukosekana kwa hali ya usafi,” anasema Ummy.Hata hivyo, anasema mkakati mkubwa uliopo sasa ni kubadilisha mwamko na mtazamo wa wananchi kwanza, lakini pia kuweka sheria kali ili watu waone umuhimu wa kuwekeza katika usafi.Waziri huyo anasema imefika wakati sasa tathmini ifanyike kwa kila kijiji kuona matokeo ya kampeni ya kitaifa ya usafi wa mazingira tangu kuanzishwa kwake mwaka 2012, ni wagonjwa wangapi wa matumbo na maradhi yatokanayo na ucha-fu wamepungua kiidadi.“Hatuwezi kuwa nchi yenye uchumi wa kati kama asilimia 40 tu ya kaya ndizo zenye vyoo bora huku kati ya shule 100 Tanzania, 28 pekee ndizo zenye vyoo bora,” anasema Ummy.

Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Suleiman Jafo anasema ofisi yake ipo tayari kuchukua kampeni hii ya usafi wa mazingira, kwa kuwa kila mkoa, wilaya, tarafa na kijiji ipo chini yake.

“Tutahakikisha kampeni hii inafanikiwa na watu wanabadili tabia zao, tuache kufanya kwa mazoea tungependa ujenzi wa vyoo bora uwe ni sehemu ya kipimo cha utendaji katika wilaya,” anasema.

Jafo anawaagiza wakurugenzi, wakuu wa wilaya na mikoa kuhakikisha wanatekeleza kwa vitendo awamu ya pili ya kampeni ya kitaifa ya usafi wa mazingira.

Anasema wakurugenzi kutenga ikama za afya zina lengo la kupata watumishi wenye kada za afya kusimamia maeneo hayo muhimu katika kutekeleza kampeni hiyo kwa asilimia 100 ifikapo 2021.

Mratibu wa huduma za maji, afya na mazingira shuleni kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi na Teklnolojia, Teresia Kuiwite anasema wizara yake kwa kushirikiana na Tamisemi wameanzisha vilabu vya mazingira katika kila shule.

“Hilo linawafanya wanafunzi watakapokuwa, waelewe nini maana ya vyoo bora.”

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, Peter Serukamba anasema kampeni hiyo ni muhimu na iwapo Taifa likiamua kupima utendaji wa wakuu wa mikoa na wilaya katika ujenzi wa vyoo, watafanikiwa.

“Kama hawatafikia malengo basi wataondolewa kwenye nafasi zao. Hili ndilo azimio. Kama Njombe wameweza, hakuna sababu kwanini wengine washindwe.”

Awamu ya pili ya kampeni 2017/2021

Awamu ya pili ya Kampeni ya Kitaifa ya Usafi wa Mazingira ilizinduliwa mjini Dodoma Desemba 7 na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan iliyowakutanisha mawaziri mbalimbali, wakurugenzi na makatibu.

“Hapa nchini asilimia 40.5 pekee ya kaya ndizo zenye vyoo bora wakati huo takwimu zinatuambia kaya laki sita hazina vyoo kabisa,” anasema hali hiyo inabainisha kiini cha kuendelea kushamiri kwa maradhi ya kuambukiza hususani kuhara na kipindupindu ambacho hadi sasa kinajitokeza katika baadhi ya mikoa na Halmashauri.

Samia Suluhu anasema madhara ya ukosefu wa miundombinu bora ya Usafi wa Mazingira hayaishii kusababisha maradhi na vifo, bali yanagusa sekta nyingine.

“Tanzania tunapoteza fedha nyingi kutokana na hali duni ya usafi hasa ukosefu wa huduma ya vyoo bora. Nchi yetu inaendelea kupambana na ugonjwa wa kipindupindu ambao hadi Novemba 12, 2017, watu 27,554 wameripotiwa kuugua na 432 walifariki dunia,” anasema.

Waziri wa Afya, Ummy anasema awamu ya kwanza ya Kampeni ya Taifa ya Usafi wa Mazingira ilianza mwaka 2012/2016 ambayo ililenga ujenzi na matumizi bora ya vyoo, ikishirikisha halmashauri 163 tu.

“Kupitia utekelezaji wa awamu ya kwanza, jumla ya kaya 519,000 zilijenga vyoo bora na tulilenga kaya 600,000, vituo vya afya 441 vimejengewa vyoo bora kutoka malengo ya vituo 250, hivyo tumefanikiwa upande huo kwa asilimia 146,” anasema Ummy.

Anasema lengo la wizara ilikuwa ni kuzifikia kaya Milioni moja kutibu maji kwa kuweka dawa au kuyachemsha, lakini zilizofikiwa ni kaya 934,437 ambazo sasa zimeanza kutibu maji sawa na asilimia 93.

Mwongozo wa huduma za maji, vituo vya tiba

Wakati wa kuelekea utekelezaji wa awamu ya pili ya kampeni hiyo, hali ya upatikanaji wa maji safi na salama pamoja na vyoo katika vituo vya kutolea huduma za afya hasa maeneo ya vijijini bado ni changamoto.

Imeelezwa ni asilimia 44 pekee ya vituo vya afya vyenye huduma hizo. Kati ya hizo, asilimia 34 ya vituo hivyo vimebainika bado vinatumia maji kutoka vyanzo visivyosalama huku asilimia 56 zikikosa kabisa uwapo wa huduma hizo muhimu.

Takwimu hizo ni kwa mujibu wa utafiti wa tathmini ya upatikanaji wa huduma muhimu katika vituo vya afya kwa mwaka 2014/15 uliofanywa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kwa kushirikiana na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto na wadau wengine.

Ili kukabiliana na hali hiyo, Serikali kupitia Wizara ya Afya, imezindua Mwongozo wa Taifa wa Huduma za Maji na Usafi wa Mazingira katika vituo vya afya.

Akizungumzia kuhusu mwongozo huo, Mratibu wa Kampeni ya Taifa ya Usafi wa Mazingira, Anyitike Mwakitalima anasema umeandaliwa kwa makusudi ya kuboresha utoaji huduma katika vituo vyote vya afya nchini.

Anasema kupitia mwongozo huo wameelekeza jinsi ya kufanya ili kuweza kufikia lengo la kuwa na vyoo bora na huduma.

Mkurugenzi wa Uratibu wa Kisekta wa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Dk Andrew Komba anasema mwongozo huo utaisaidia Serikali na wadau wa maendeleo kusimamia na kutekeleza masuala ya usafi wa mazingira katika maeneo hayo.

“Mwongozo unatoa maelekezo stahiki wa namna vituo vya afya katika ngazi zote vinavyopaswa kufanya kwenye upangaji mipango na uandaaji wa bajeti zitakazotumika kusimamia usafi wa mazingira,” anasema.

Naye Mkurugenzi wa Mipango wa Shirika la WaterAid, Abel Deganga anasema kutokana na kukosekana kwa mwongozo kwa muda mrefu unaopima hali ya upatikanaji wa maji kwenye vituo vya afya nchini, utendaji kazi wa Serikali na wadau ambao ulikuwa unasuasua.