Mongella ‘awananga’ wanaotaka Ikulu

“Tuwe wakweli katika hili. Siku zote hatusemi ukweli, hatuwaambii ukweli wananchi...”
Getrude Mongella

Muktasari:

Mwanasiasa huyo mkongwe nchini alisema, “Watu wanapanda jukwaani na kuwadanganya wananchi mambo mbalimbali lakini lengo ni kuingia Ikulu.

Dar es Salaam. Mbunge wa zamani wa Ukerewe, Getrude Mongella amewananga baadhi ya wanasiasa kuwa si wazalendo, hawana maadili na wanatumia njia zisizopendeza kuwahadaa wananchi ili waingie Ikulu.

Mongella aliyekuwa Mwenyekiti wa Mkutano wa Kimataifa wa Wanawake, uliofanyika Beijing, China 1995, aliyasema hayo mwishoni mwa wiki katika Kongamano la Viongozi kujadili changamoto za kuongoza mabadiliko lililoandaliwa na Uongozi Institute.

Mwanasiasa huyo mkongwe nchini alisema, “Watu wanapanda jukwaani na kuwadanganya wananchi mambo mbalimbali lakini lengo ni kuingia Ikulu.

“Tuwe wakweli katika hili. Siku zote hatusemi ukweli, hatuwaambii ukweli wananchi na kila siku akili za wengi ni kuitaka Ikulu wakati hawana hata ‘background’ ya nchi hii, tunatenda dhambi.”

Alisema viongozi wengi si wazalendo, wameibuka tu. “Viongozi wengi ni wa kufumba na kufumbua tayari wamekuwa viongozi, hawana uzalendo kabisa, na hawajui wanachokifanya na ndiyo maana maadili yanaporomoka.”