Baleke aanza na mkwara Simba

Muktasari:

  • Jean Beleke alisajiliwa na Simba kwa mkataba wa miaka miwili akitokea TP Mazembe huku akisema amekuja kuongeza makali kikosini hapo.

Mshambuliaji mpya wa Simba, Jean Baleke atakuwa sehemu ya kikosi cha timu hiyo kitakachoanza mazoezi mara baada ya kumalizana na mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Mbeya City, huku akichimba mkwara.
Kabla ya kutua nchini Baleke aliyesajiliwa akitokea TP Mazembe, ameliambia Mwanaspoti kuwa anakuja kuongeza makali ya Simba haswa kwenye eneo la kufunga na amepanga kulifanya hilo ili kuhakikisha timu inafanya mashindano yote.
Baleke alisema kabla ya kufanya maamuzi ya kujiunga na Simba anafahamu aina ya wachezaji wao wote na wale wanaocheza kwenye safu ya ushambuliaji ambayo anaitumikia.
Alisema anamfahamu, John Bocco kabla ya kuja Tanzania aliweza kumfuatilia na kugundua kuwa anajua kufunga na msimu huu amefunga mabao tisa, hadi sasa ingawa mwanzoni hakuanza vizuri.
“Moses Phiri mwenye mabao kumi namfahamu na wachezaji wengine kama Clatous Chama naelewa wapo kwenye viwango bora ila naamini nikiongezeka na mimi tutakuwa na uimara zaidi ya wakati huu,” alisema Baleke na kuongeza;
“Kabla ya kusajili nilimwambia kiongozi (Jina lake tunalo), sitamani tena kucheza TP Mazembe, nataka kuja Simba ili kuonyesha makali yangu haswa kwenye eneo la kufunga ili timu iweze kufanikiwa kwenye mashindano mbalimbali ya ndani na kimataifa,”
“Naamini kwenye ushindani na changamoto ya kuwania nafasi ya kucheza, wachezaji wanaotumika kwenye eneo hilo la ushambuliaji kila mmoja atakayeonyesha uwezo wake mazoezini naimani benchi la ufundi litatoa nafasi kwa aliyefanya vizuri,”
“Kuna kitu ninacho kwenye uwezo wangu hadi Simba kuvutiwa kunisajili basi nitakwenda kupambana na naamini nitaweza kupata nafasi ya kucheza kwenye kikosi cha kwanza mara kwa mara.
“Siwezi kueleza nitamaliza na msimu nikiwa na mabao mangapi ila jambo kubwa nakuja kuisaidia timu na kufanya vizuri katika kila mechi ambayo nitapata nafasi ya kucheza na hilo naamini linawezekana.
“Ukiangalia ubora na aina ya wachezaji wa Simba naamini tunakwenda kufanya vizuri kwenye mashindano ya kimataifa ndiyo maana nikakubali kujiunga nao.
Katika hatua nyingine, Baleke alisema alipata nafasi ya kuangalia baadhi ya mechi za mashindano ya ndani timu mbalimbali anazifahamu kama Yanga na Azam na aina ya wachezaji waliyokuwa nao.
“Namuomba Mungu anitangulie kwenye changamoto hii mpya ila kwani malengo yangu ni kuja kufanya vizuri na kuipa mafanikio timu pamoja na furaha kwa mashabiki wake, nimewaona Azam na Yanga na nawafahamu wote,” alisema Baleke aliyewahi kuifunga Simba kwenye mechi ya kirafiki Uwanja wa Benjamin Mkapa akiwa na TP Mazembe.