Guardiola atoa tahadhari Man City ikiingia Bernabeu
Meneja wa Manchester City, Pep Guardiola, ambaye amewapa tahadhari wachezaji wake kuelekea katika mechi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Real Madrid. Picha na Mtandao
Muktasari:
- Katika mechi tazo zilizopita baina yao, Real Madrid imeshinda mara mbili, Man City ikishinda mara moja huku timu hizo zikitoka sare mbili.
Meneja wa Manchester City, Pep Guardiola, amewataka wachezaji wake kucheza kwa kujiamini watakapokutana na Real Madrid katika mchezo wa hatua ya 16 bora ya Ligi ya Mabingwa Ulaya.
Mchezo huo wa mkondo wa kwanza unatarajiwa kuchezwa leo Jumatano Machi 11, 2026 katika uwanja wa Santiago Bernabéu, huku Guardiola akisisitiza kuwa njia pekee ya Man City kufuzu robo fainali ni kucheza kwa mtindo wao wa kawaida.
Kocha wa Manchester City, Pep Guardiola, wakati akizungumza na wanahabari kabla ya mechi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Real Madrid. Picha na Mtandao
“Mambo mazuri hayawezi kutokea kama huna utambulisho wako. Lazima tucheze kama timu,” amesema Guardiola.
Manchester City na Real Madrid zimekutana mara nyingi katika miaka ya hivi karibuni kwenye michuano hii ambapo katika mechi tazo zilizopita Real Madrid imeshinda mara mbili, zikitoka sare mara mbili huku Man City ikishinda mara moja.
Majeraha Real Madrid
Real Madrid wanaingia katika mchezo huo wakiwa na nuksi ya majeraha kwa baadhi ya nyota wao akiwemo Kylian Mbappé na Jude Bellingham, hali inayoweza kuwapa nafuu Man City.
Kipa wa Man City, Gianluigi Donnarumma amesema kutokuwepo kwa Mbappe kunaweza kupunguza hatari kwa safu yao ya ulinzi.
“Nimewahi kucheza na Mbappe, ni mmoja wa wachezaji bora duniani. Kutokuwepo kwake kunaweza kuwa faida kidogo kwa kipa,” amesema.
Baadhi ya nyota wa Manchester City, wakijifua katika Uwanja wa mazoezi kabla ya mchezo wa Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya Real Madrid. Picha na Mtandao
Tucheze bila hofu
Guardiola amesema wachezaji wake hawapaswi kuogopa presha ya kucheza katika uwanja wa Bernabeu, bali wanapaswa kucheza kwa ujasiri kama walivyofanya walipoifunga Newcastle katika Kombe la FA mwishoni mwa wiki iliyopita.
“Jaribuni kucheza vizuri kuliko wapinzani wenu. Kama tukitolewa, basi tuwapongeze Real Madrid lakini angalau tutakuwa tumecheza kwa utambulisho wetu,” amesema Guardiola.
Mchezo huo unatarajiwa kuwa mkali huku kila timu ikisaka ushindi wa awali kabla ya mchezo wa marudiano utakaochezwa England.
Mechi nyingine zitakazopigwa leo ni kati ya PSG itakayokuwa nyumbani kuikaribisha Chelsea, Arsenal itakuwa ugenini dhidi ya Bayer Leverkusen wakati Bodo/Glimt watakuwa nyumbani kuvaana na Sporting CP.