Hadithi ya huzuni ya mshambuliaji wa Iraq
Muktasari:
- Nyota huyo aliandika rekodi ya kuifungia timu yake bao la kwanza katika Fainali za Kombe la Dunia 2026.
Aymen Hussein juzi aliifungia Iraq bao pekee katika kichapo walichokipata cha mabao 4-1 kutoka kwa Norway lakini nyuma ya bao hilo, kuna historia ya kusikitisha kwa nyota huyo wa Iraq.
Akiwa na umri wa miaka 12 mwaka 2008, baba yake ambaye alikuwa mwanajeshi katika jeshi la Iraq aliuawa kwa kupigwa risasi na kundi la Wanamgambo wa Al-Qaeda wakati alipokuwa akienda kununua vifaa vya ujenzi wa nyumba yao.
Miaka michache baadaye, kaka yake mkubwa alitekwa nyara katika kipindi cha machafuko na hajawahi kuonekana tena hadi sasa.
"Niliamua kuacha kucheza soka ili niweze kuitunza familia yangu, lakini mama yangu alikataa," alisema Hussein katika mahojiano.
Badala yake, mama yake alimhimiza Hussein kuendelea na ndoto yake ambayo hatimaye imemwezesha kuiongoza Iraq kufuzu Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza tangu mwaka 1986.
Hata hivyo, safari ya kufikia mafanikio hayo haikuwa rahisi kwa mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 30.
Maandalizi ya Hussein kuelekea Kombe la Dunia yalitatizwa aliposhikiliwa na kuhojiwa kwa takribani saa saba katika uwanja wa ndege wa O'Hare jijini Chicago baada ya kuwasili nchini Marekani mapema mwezi huu.