Lindi yapanda miti milioni moja kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi
Mkuu wa mkoa wa Lindi Zainab Telack akipanda mti wa kivuli katika shjle ya sekondari ya kanda kiwalala iliyopo Halmashauri ya Mtama ,kuelekea katika siku ya misitu duniani ambapo kitaifa inafanyika mkoani Lindi.Picha na Bahati Mwatesa
Muktasari:
- Mkoa wa Lindi wapanda miti zaidi ya milioni moja katika kampeni ya kitaifa ya upandaji miti na kuelekea maadhimisho ya siku ya misitu duniani.
Mtama. Jumla ya miti milioni moja na laki mbili imepandwa katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Lindi, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha uhifadhi na utunzaji wa misitu kuelekea maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani pamoja na kampeni ya kitaifa ya upandaji miti.
Akizungumza mara baada ya zoezi la kupanda miti katika shule ya sekondari ya kanda ,kiwalala Halmshauri ya Mtama leo, Machi 17, 2026, Mkuu wa Mkoa wa Lindi, Zainab Telack, amewataka wananchi wa mkoa wa Lindi,kuendelea kutunza misitu ili kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.
Amesema kuwa Mkoa wa Lindi ni miongoni mwa maeneo yaliyobaki na misitu, hivyo ni muhimu kuilinda ili kuepuka athari za ukame na upungufu wa mvua.
“Sisi tumebaki na misitu, tukiamua kuendelea kukata miti hovyo tuliyonayo, tutaishi maisha magumu kwa sababu tutasababisha mkoa wetu kubaki jangwa na tutakosa mvua,” amesema Telack.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Misitu na Nyuki kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, Daniel Charles,ameweka wazi kuwa wizara kupitia Wakala wa Huduma za Misitu(TFS) imeweka kipaumbele katika kuelimisha na kuhamasisha jamii kuhusu upandaji miti.
Ameongeza kuwa kampeni ya kitaifa ya upandaji miti ilianza Januari 2026, ambapo hadi sasa miti milioni mia moja na kumi na tatu elfu imepandwa katika maeneo mbalimbali nchini na kwa Mkoa wa Lindi pekee, miti milioni moja na laki mbili tayari imepandwa.
"Hadi sasa miti zaidi ya milioni mia moja na kumi imepandwa katika maeneo mbalimbali nchini,ambapo mkoa wa Lindi pekee miti milioni moja na laki mbili tayari imepandwa."amesema Charles.
Mwanafunzi wa kidato cha pili kutoka shule ya sekondari Kiwalala Jafari Mahamudu ameishukuru Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kuweza kuhamasisha wananchi katika zozi la upandaji miti ambapo pia wameahidi kuitunza miti hiyo ambayo itasaidia kizazi cha sasa na kizazi kijacho.
"Tunashukuru Wizara ya Maliasili na Utalii kuweza kuja shuleni kwetu kutupandia miti ya matunda pamoja na miti ya kivuli,niahidi kwa niaba ya wanafunzi wenzangu tutaitunza ipasavyo ili ije kuwasaidia wadogo zetu na kizazi kijacho."amesema Mahamudu.