Mgombea DP amtaja Mchungaji Mtikila, akiahidi kuwafuta machozi walalahoi
Muktasari:
- Kwa upande wa watumishi ameahidi neema kila atakayeajiriwa atafanya kazi kwa mwaka mmoja na baada ya hapo atakopeshwa nyumba ili kuwapunguzia watumishi mawazo.
Dodoma. Chama Cha DP leo Jumatano Agosti 13,2025 kimejitofautisha na vyama vingine kilipofika kuchukua fomu kwa mgombea wao wa kiti cha urais.
Tofauti na vyama vingine kilikuwa na idadi ndogo ya watu walioingia katika jengo la ofisi ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), pia walitumia gari moja.
Mbali na uchache huo, lakini mgombea wa chama hicho Abdul Mluya anakuwa mtu wa kwanza aliyeingia na gari isiyokuwa na bendera wala nembo ya chama.
Nje ya uzio kulikuwa na pikipiki nane ambazo zilitumika kuwabeba makada hao hadi watatu kwenye chombo kimoja.
Hata hivyo mara baada ya kukabidhiwa fomu, mgombea Mluya amekuwa wa kwanza kuzungumza maneno mengi ukilinganisha na waliomtangulia, huku akimtaja Mchungaji Christopher Mtikila.
"Mchungaji Mtikila alikufa akipigania haki, nasi leo tunataka haki na sisi ndiyo chama pekee cha kwenda kuwafuta machozi walalahoi," amesema Mluya.
Amesema DP kinalaani maiti kugeuzwa pato la Taifa badala yake kila msiba utakaotokea lazima ndugu wakabidhiwe bila kudai malipo ya aina yoyote na iwe kwa haraka.
Kwa upande wa watumishi ameahidi neema kila atakayeajiriwa atafanya kazi kwa mwaka mmoja na baada ya hapo atakopeshwa nyumba ili kuwapunguzia watumishi mawazo.
"Kubwa kuliko yote ni kuboresha pato la watumishi na kufuta mambo ya kikokotoo ambacho kimekuwa kilio namba moja kwa watumishi Tanzania," amesema.
Kingine ametaja kufanya maboresho makubwa ndani ya Jeshi la Magereza ili kuweka nidhamu ya kutosha kwa askari wake ambao amedai maisha yao hayana tofauti na wafungwa.