Shincheonji yaadhimisha miaka 42, waumini wahimizwa kushikamana na neno
Mwenyekiti Lee Man-hee akihutubia waumini wakati wa ibada ya maadhimisho ya miaka 42 ya kuanzishwa kwa Shincheonji Kanisa la Yesu, iliyofanyika katika Kanisa la Cheongju, Korea Kusini.
Dar es Salaam. Kujitolea kwa waumini wa mwanzo wa Shincheonji Kanisa la Yesu, walioanza ibada katika ghorofa ya chini ya nyumba miaka 42 iliyopita, kumezaa uamsho mkubwa wa kiroho unaovutia maelfu ya waumini kutoka mataifa mbalimbali kila mwaka.
Hayo yamesemwa na Mwenyekiti wa kanisa hilo, Lee Man-hee, wakati wa ibada ya maadhimisho ya miaka 42 tangu kuanzishwa kwa dhehebu hilo la Kikristo lenye makao yake makuu Korea Kusini.
Ibada hiyo ililenga kutoa shukrani kwa kujitoa kwa Yesu, mashahidi na waanzilishi wa imani waliotangulia, sambamba na kuimarisha msimamo wa ‘imani inayozingatia Neno’.
Zaidi ya waumini 2,000 walishiriki ibada hiyo ana kwa ana, huku wengine kutoka ndani na nje ya Korea Kusini wakifuatilia kupitia matangazo ya moja kwa moja mtandaoni.
Akihutubia waumini, Lee amewahimiza kujikita katika imani ya kweli inayotokana na Neno la Mungu.
“Kama Yohana 1:1 inavyosema kwamba Neno ni Mungu, basi haiwezekani kuwa na imani bila Neno. Leo tunapoadhimisha miaka 42, tukusanye mioyo yetu na kujitahidi kuwa na imani inayokubalika mbele za Mungu na malaika,” amesema.
Aidha, amesisitiza umuhimu wa kushikamana na mafundisho ya Kitabu cha Ufunuo, akionya dhidi ya kuongeza au kupunguza yaliyomo ndani yake.
“Ufunuo 22 unaonya kwamba yeyote anayeongeza au kupunguza katika kitabu hiki hatapata uzima wa milele. Kila muumini anapaswa kujichunguza kama anafuata Neno kikamilifu,” ameeleza.
Baadhi ya waumini wa muda mrefu walioshiriki ibada hiyo walieleza namna walivyoshuhudia ukuaji wa kanisa hilo.
Bak Bok-yeong (70), aliyekuwapo hata kabla ya kuanzishwa rasmi kwa kanisa hilo, alisema aliona ndoto yake ya kuelewa Neno la Mungu ikitimia.
“Ilikuwa furaha kubwa kuona kiu yangu ya Neno ikijibiwa. Leo ninapoona maelfu ya watu wakimiminika kila mwaka, ninaamini ni nguvu ya Neno inayogusa mioyo yao,” amesema.
Naye Jo Myeong-suk (73), aliyejiunga mwaka 1992, alisema alivutiwa na mafundisho ya kina ya Biblia yaliyomfanya kuchukua uamuzi wa kujiunga na kanisa hilo.
“Nilikuwa natafuta uhakika wa wokovu na uelewa wa kweli wa Biblia. Nilichokipata hapa kilikuwa cha kipekee na kilinifanya niwe sehemu ya imani hii,” amesema.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Shincheonji ilianzishwa Machi 14, 1984, na imeendelea kupanuka duniani kupitia shughuli zake za uinjilisti na elimu ya Biblia, hususan kupitia Kituo cha Misheni cha Kikristo cha Sayuni.