Watanzania walivyonufaika na Kombe la Dunia
Kampuni ya huduma za fedha kidijitali Mixx imetangaza kuwa droo ya mwisho ya kampeni ya "Ikiingia Tu Goli" itafanyika wiki ijayo, ambapo mshindi mmoja atajishindia Shilingi milioni 50.
Akizungumza wakati wa kukabidhi zawadi kwa washindi wa droo ya tisa ya kampeni hiyo inayofanyika kwa ushirikiano na Hisense, Mkuu wa Idara ya Makampuni na Washirika - Mixx, Justine Lawena, alisema kampeni hiyo imeendelea kuwahamasisha Watanzania kutumia huduma za kifedha kidijitali huku ikiwazawadia fedha taslimu na vifaa mbalimbali.
Katika droo hiyo, washindi 10 walipatikana, ambapo saba walijishindia shilingi milioni moja kila mmoja, huku watatu wakijishindia vifaa vya Hisense. Lawena alisema hadi sasa kampeni hiyo imewazawadia zaidi ya Watanzania 90 tangu ilipoanza.
"Fainali za Kombe la Dunia zimekwisha, lakini fainali ya kampeni yetu ndiyo inafuata wiki ijayo. Hapo ndipo tutampata mshindi wa shilingi milioni 50. Bado kila Mtanzania ana nafasi ya kushinda kwa kutumia Mixx Super App," alisema Lawena.
Alisema ili kushiriki droo ya mwisho, mteja anatakiwa kutumia Mixx Super App kufanya miamala kama kutuma na kupokea fedha, kulipa bili na kufanya malipo ya Serikali.
Lawena aliwataka wateja kuwa makini wanapopigiwa simu kutoka namba 100, akieleza kuwa hiyo ndiyo namba rasmi ya kuwataarifu washindi.
"Tunawakumbusha wateja kupokea simu kutoka namba 100. Usipoipokea unaweza kupoteza fursa ya kuthibitisha ushindi wako. Bado una nafasi ya kushinda kwa kuendelea kutumia Mixx Super App," alisema.
Mmoja wa washindi wa Shilingi milioni moja, Bw. David Kisusi, alisema ushindi huo umempa motisha zaidi kuendelea kutumia Mixx kutokana na urahisi na usalama wa huduma zake.
"Nimekuwa nikitumia Mixx kwa shughuli zangu za kila siku na ninaweza kulipia bili mbalimbali kwa urahisi kupitia simu yangu. Kinachonivutia zaidi ni usalama wa huduma hizi, kwani hata muamala unapokwenda kimakosa, kuna msaada wa haraka wa kuuzuia au kuurejesha," alisema Kisusi.