Apandishwa kizimbani kwa kumkashifu Rais Magufuli

Muktasari:

Sarehe amesema mshtakiwa alitenda kosa hilo kinyume na kifungu cha sheria namba 89 (1) ya mwaka 2002.


Misungwi. Mkazi wa Wilaya ya Ngara, Kagera Justin Emmanuel (31)   amefikishwa Mahakama ya Wilaya Misungwi mkoani Mwanza, kwa tuhuma ya kutoa lugha chafu dhidi ya Rais John Magufuli.

Mwendesha mashtaka wa polisi Ramsoney Sarehe alisoma hati ya mashtaka mbele ya ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa mahakama hiyo, Erick Marley leo Julai 3.

Sarehe amesema mshtakiwa alitenda kosa hilo kinyume na kifungu cha sheria namba 89 (1) ya mwaka 2002.

Amesema mshtakiwa alitoa lugha ya kumdhihaki Rais Juni 25 katika Kivuko cha Kigongo saa 10:00 jioni kwa kutamka maneno ya “Rais kitu gani bwana”.

Hata hivyo mshtakiwa alikana kosa hilo na hakimu aliahirisha shauri hilo hadi Julai 26 itakapotajwa tena mahakamani.

Mshtakiwa yupo nje kwa dhamana baada ya kukamilisha masharti ya kuwa na mdhamini mmoja aliyewasilisha bondi ya mali isiyohamishika yenye thamani ya Sh500, 000.