Salamba: Nimenyoa rasta sababu ya wazazi

Muktasari:

Mtanzania anayekipiga Al Jahra ya nchini Kuwait, Adam Salamba anapenda kuishi kulingana na mazingira, kitu kilichomfanya anyoe rasta zake baada ya kurejea kwao Shinyanga.

MAISHA ya Adam Salamba anayekipiga Al Jahra FC ya Kuwait, akiwa kazini ni tofauti na anaporejea nyumbani kwa wazazi wake kama anavyosimulia mwenyewe.
Mwonekano wake kichwani anapendelea kufuga rasta, lakini hivi karibuni amenyoa ambapo MCL Digital limezungumza naye kujua nini kipo nyuma ya pazia na kupelekea kuwa na mwonekano mwingine.
Hakusita kuweka wazi kwa nini ameamua kunyoa rasta zake kwamba anarejea kwa wazazi wake likizo hivyo hawezi kwenda na mwonekano ambao watakuwa wanamshangaa.
"Huwa sipendi kwenda nyumbani nikiwa na nywele za kufuga kwa sababu ninakwenda kukutana na watu wa kila aina hasa watu wazima, hivyo sipendi wawe wananiangalia kama mhuni,"
"Hakuna anayenikataza kuwa na rasta nyumbani, ila lazima nijue kuishi kulingana na mazingira, uzuri wa nywele zangu zinakua haraka, nikirejea kazini nitazifuga tena,"amesema.
Mbali na hilo amezungumzia kazi yake kwamba mpaka sasa amefikisha mabao manne, tangu ajiunge na timu hiyo akitokea Namungo ambako alipelekwa kwa mkopo na Simba.
"Ndio nimeanza kurejea kwa sababu nilikuwa nasumbuliwa na majeraha, nimecheza mechi saba, nimefunga mabao manne, ila kwenye mechi za kirafiki nimefunga mabao mengi  zaidi," amesema.