Kocha Eymael alia mwamuzi Saanya kuinyima penalti Yanga

Muktasari:

Kocha Eymael tangu ametua nchini mara kwa mara amekuwa kizozana na waamuzi akiwalaumu kwa kushindwa kuchezesha kwa haki.

Dar es Salaam.Kocha wa Yanga, Luc Eymael ameendelea kulumbana na waamuzi akisema hafurahishwi na namna wanavyochezesha Ligi Kuu Tanzania Bara.

Akizungumza baada ya kuishuhudia Yanga ikilazimishwa sare 1-1 na Mbeya City, Mbelgiji Eymael alimshushia lawama mwamuzi Martin Saanya kwa kuinyima penalti timu yake baada ya Benard Morrison kufanyiwa madhambi ndani ya boksi.

"Sikusema haya katika mchezo uliopita, lakini leo nasema, ile faulo aliyofanyiwa Morrison haikustahili kuwa penalti? alihoji kocha huyo.

Luc alisema hali hii inafanya wakosekane waamuzi wa Tanzania kuchezesha mashindano ya Afrika Afcon.

"Lini hapa aliwahi kuchaguliwa mwamuzi wa Tanzania kwenda Afcon? hakuna bila shaka eeh ndio hakuna," alisema Mbelgiji huyo.

Waamuzi wengi wamekuwa katika wakati mgumu hivi karibuni baada ya kutoa uamuzi yenye utata katika michezo kadhaa ya Ligi Kuu Tanzania Bara.