Solskjaer ataka straika mpya Man United

Muktasari:

  • Kocha wa Manchester United, Ole Gunnar Solskjaer anataka mshambuliaji mpya kujaza nafasi ya Romelu Lukaku aliyejiunga na Inter Milan

London, England. Ole Gunnar Solskjaer anataka mshambuliaji mpya katika kikosi cha Manchester United kwenye usajili wa dirisha dogo Januari, mwakani.

Solskjaer amewapoteza washambuliaji Romelu Lukaku na Alexis Sanchez waliojiunga na Inter Milan katika usajili wa majira ya kiangazi.

Kocha huyo amewaeleza vigogo wa bodi ya klabu hiyo anataka mshambuliaji mwenye kiwango bora cha kufunga mabao Man United.

“Ndio tumewapoteza Alexis na Romelu, tunahitaji mshambuliaji mbunifu mwenye kiwango  bora cha kufunga mabao,” alisema Solskjaer.

Nguli huyo wa zamani wa timu hiyo alisema hakuna na namna zaidi ya kumpiga bei Lukaku kwa kuwa hakutaka kubaki Old Trafford.

Kocha huyo alisema safu yake ya ulinzi inafanya vyema, lakini hana furaha na namna washambuliaji wanavyocheza.

Man United imefunga mabao manne katika mechi tano na moja tu ndio ilitoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Rochdale ya daraja la kwanza katika Kombe la Ligi kabla ya kushinda kwa penalti.

Lukaku alifunga mabao 42 katika misimu miwili Man United na sasa amefunga matatu katika mechi sita Inter Milan.