Swizz Beats amuomba Diamond wimbo wa Gere

Muktasari:

Mtayarishaji maarufu wa muziki nchini Marekani, Swizz Beats amemuomba msanii wa Tanzania, Diamond Platnumz kumtumia wimbo wake mpya wa Gere.

Dar es Salaam. Mtayarishaji maarufu wa muziki nchini Marekani, Swizz Beats amemuomba msanii wa Tanzania, Diamond Platnumz kumtumia wimbo wake mpya wa Gere.

Diamond ameuweka wimbo huo leo Jumatano Februari 19, 2020 katika mtandao wa Youtube na ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram.

Katika Instagram, kipande cha wimbo huo kimewekwa leo saa 6 mchana lakini hadi saa 10:20 jioni ulikuwa umetazamwa mara 171,005.

Katika Youtube, hadi saa 10:26 ulikuwa umetazamwa mara 425,178.

Beatz ambaye jina lake halisi ni Kasseem Dean aliandika ujumbe katika ukurasa wa Diamond wa Instagram, akimuomba amtumie wimbo huo, Diamond amekubaliana na ombi hilo.

Mtayarishaji huyo maarufu wa muziki ambaye ni mume wa msanii Alicia Keys ameshawatengenezea nyimbo wanamuziki maarufu  nchini Marekani akiwemo Beyonce katika wimbo wa Check on It na Ring the Alarm.

Nyimbo nyingine alizozitengeneza ni Jigga My Nigga na  Girl's Best Friend  za Jay-Z; Ultralight Beam wa Kanye West;  Touch It wa Busta Rhymes; Party Up (Up in Here) wa  DMX na Gotta Man wa Eve E.