Wimbo Dodo wazua jambo Youtube, meneja wa Ali Kiba azungumza

Muktasari:

Esi Mgimba ambaye ni meneja wa msanii wa Tanzania, Ali Kiba amezungumzia watazamaji wa wimbo Dodo wa msanii huyo katika mtandao wa Youtube kushuka kutoka milioni moja hadi 750,000.

Dar es Salaam. Esi Mgimba ambaye ni meneja wa msanii wa Tanzania, Ali Kiba amezungumzia watazamaji wa wimbo Dodo wa msanii huyo katika mtandao wa Youtube kushuka kutoka milioni moja hadi 750,000.

Wimbo huo ambao Ali Kiba amemtumia  mwanamitindo, Hamisa Mobetto kama mpamba video uliachiwa Youtube juzi Jumatano Aprili 8, 2020 na kutazamwa na watu milioni moja ndani ya saa 24 lakini jana jioni walioutazama walishuka na kufikia 750,000 kitu ambacho kiliibua hali ya sintofahamu.

Akizungumzia hali hiyo katika ukurasa wa mtandao wake wa kijamii wa Instagram, meneja huyo amesema, “haijalishi mara ngapi akaunti za YouTube za baadhi ya watu zinachezewa, inakera na hata wakituchezea wakae wajue halitaondoka Dodo.”

"Ila isitukatishe tamaa kufanya muziki mzuri na kuupigania hata wakifanyaje zitarudi, zitaongezeka  na bado tunaongeza vingine dawa ikolee, haanguki mtu hapa.”

Hata hivyo, leo Ijumaa Aprili 10, 2020 idadi ya walioutazama wimbo huo ni zaidi ya milioni moja.