Tanzania kuandaa kongamano la biashara la Tanzania-Uganda

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dk Damas Ndumbaro

Muktasari:

Tanzania inatarajiwa kuwa mwenyeji wa kongamano la wafanyabiashara kati ya Tanzania na Uganda litakalofanyika Septemba 3 hadi 5 mwaka huu jijini Dar es Salaam.

Dar es Salaam. Taasisi ya Sekta binafsi Tanzania (TPSF)  inaandaa kongamano la kibiashara kati ya Tanzania na Uganda litakalofanyika jijini Dar es Salaam ambapo pamoja na mambo mengine litawezesha kuwaunganisha wafanyabiashara.

Kufuatia kongamano hilo, Serikali imeishauri TPSF kushirkikiana na wenzao wa Uganda kuchangamkia fursa zinazotolewa na mradi mkubwa wa reli ya kisasa (SGR) na nyinginezo.

Kauli hiyo ilitolewa jana na naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dk Damas Ndumbaro alipokuwa akizindua mwanzo wa kongamano litakalofanyika Septemba mwaka huu.

Alieleza kuwa Tanzania inazo fursa nyingi ukiwemo mradi wa reli ya kisasa unaweza kusafirisha mizigo kwa treni na kufika Uganda au kutumia bandari ya Dar es Salaam kwa ajili ya kufanikisha biashara katika nchi hizo mbili.

“Kuna fursa nyingi ambazo sekta binafsi zikiwemo za sekta ya utalii, kufundisha Kiswahili Uganda pamoja na fursa nyinginezo,’” alisema.

Kwa kuzingatia hilo, alisema Serikali za Tanzania na Uganda zimeandaa kongamano hilo litakalosimamiwa na TPSF ambapo kutakuwa na maonyesho ya biashara na kuwakutanisha wafanyabiashara.

Alisema kongamano hilo litakuwa ni fursa adhimu kwa nchi zote mbili na kutafuta suluhisho za vikwazo vya biashara kati ya nchi hizo na kuanzisha majukwaa ya ushirikiano yatakayowezesha kupeana uzoefu miongoni mwa wafanyabiashara.

kwa upande wake, Mkurugenzi wa TPSF, Godfrey Simbeye alisema Tanzania inazo fursa nyingi zinazotakiwa kufanyiwa kazi. Alisema kongamano hilo litakalofanyika Septemba 3 hadi 5 mwaka huu ni fursa ya kampuni za Tanzania kutafuta uwekezaji nchini Uganda.

“Serikali imejitahidi kuboresha mazingira ya biashara ikiwa pamoja na kutekeleza mapendekezo ya Blueprint na kupunguza iliyopunguza wingi wa ushuru zilizokuwa kikwazo kwa wafanyabiashara, kwa hiyo sasa ni wakati wetu wa kuchangamkia hizo fursa hizo zilizopo,” alisema Simbeye.

Kwa upande wake Balozi wa Uganda nchini, Richard Tumisime alisifia mkakati huo wa kuziweka pamoja sekta binafsi za Tanzania na Uganda.

“Kuna fursa nyingi katika uwekezaji wan chi na nchi ambao kama utatumika utazinufaisha nchi hizi mbili,” alisema.