Bundi atua bungeni, Spika atoa neno

Spika Job Ndugai 

Muktasari:

Bundi ameonekana leo ndani ya ukumbi wa Bunge jijini Dodoma lakini Spika, Job  Ndugai amewatoa hofu bungeni kuwa Bundi wa mchana hana madhara.


Dodoma. Huwezi amini lakini ndivyo ilivyokuwa kwamba bundi leo Jumanne Januari 29, 2019 amefungua mkutano wa Bunge.

Ni ndege aliyeonekana leo asubuhi ndani ya ukumbi wa Bunge ambako kila mbunge na watumishi wa chombo hicho cha Dola waliowahi kuingia walimuona ndege huyo.

Watumishi wa Bunge waliingia ndani ya jengo hilo kwa ajili ya ukaguzi na kumuona ndege huyo juu ya paa la ukumbi wa Bunge.

Ndege huyu hakutoka licha ya maofisa hao kutaka kumtoa, aliruka kutoka sehemu moja kwenda nyingine.

Hata hivyo, haikujulikana  muda aliotoka na mahali alikoelekea lakini Spika Job Ndugai akasema ni mambo ya kawaida kwa Dodoma.

"Waheshimiwa wabunge, asubuhi tumeanza kumwona Bundi ndani ya jengo hili, lakini kwa Dodoma Bundi wa mchana hana madhara kwa hiyo ni mambo ya kawaida kabisa," amesema Ndugai.

Kauli ya Spika ni kama iliwapoza watumishi ambao walionekana kuwa na hofu juu ya ujio wa ndege huyo ndani ya jengo la Bunge.