Waziri Bashungwa atauweza mfupa uliowashinda wenzake?

Waziri wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa 

Muktasari:

Waziri wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa anakabiliwa na kazi ngumu ya kuuza korosho takriban tani 200,000 za mwaka jana zinazodaiwa kupoteza ubora baada ya kucheleweshwa kuuzwa, ikiwa ndiyo kosa lililosababisha mtangulizi wake, Joseph Kakunda kuenguliwa kwenye nafasi hiyo.


Dar es Salaam. Wakati tayari mawaziri watatu wakiwa wameshaenguliwa kutokana na sakata la korosho, Waziri wa sasa wa Viwanda na Biashara, Innocent Bashungwa anakabiliwa na kibarua kigumu kuuza takribani tani 200,000 za korosho zilizovunwa katika msimu wa mwaka 2018 huku zikionekana kupoteza ubora wake.

Mawaziri walioenguliwa na Rais John Magufuli kutokana na korosho hizo ni pamoja na aliyekuwa Waziri wa Kilimo, Dk Charles Tizeba, aliyekuwa Waziri wa Viwanda na Biashara, Charles Mwijage na hivi karibuni, mrithi wake, Joseph kakunda, wakidaiwa kushindwa kusimamia wizara zao hususani mauzo ya korosho.

Akizungumza hivi karibuni baada ya kumwapisha Waziri Bashungwa, Iklulu Dar es Salaam, Rais John Magufuli alieleza jinsi Waziri Kakunda na mamlaka za wizara hiyo zilivyoshindwa kuuza korosho, huku akiipongeza Wizara ya Kilimo na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kwa kukusanya korosho zote kwenye maghala.

Kibarua kinachomkabili Waziri Bashungwa ni kushuka kwa ubora wa korosho kwa sababu ya kukaa muda mrefu, huku nchi nyingine nazo zikiwa na korosho mpya iliyovunwa kati ya Machi na Aprili, 2019.

Ili kuepuka hasara ya moja kwa moja, Waziri Kivuli wa Viwanda na Biashara ambaye pia ni Mbunge wa Ndanda (Chadema), Cecil Mwambe ameishauri Serikali kuziuza korosho hizo kwa bei ya hasara, ili isikose kabisa.

Alisema kwa sasa korosho za Tanzania zimeshapoteza ubora wake ukilinganisha na korosho za Ghana (new stock).

“Wanapopima ubora wanaangalia nut count (hesabu ya korosho) kutokanana na unyaufu. Korosho bora zinatakiwa ziwe 150, zikinyauka zinapungua umbo na zinaingioa 170.

“Wanaangalia pia ladha ya korosho na thamani ya maganda yake kwani yanapokuwa mabichi yanaweza kutengeneza bidhaa nyinghine, lakini yakikauka, mnunuzi atapata korosho peke yake,” alisema Mwambe

Mwambe alisema bei ya korosho kwenye soko la dunia ni Sh2,600, lakini wanunuzi wanataka kununua kwa Sh1,200 ili wakichanganya na gharama za usafirishaji na nyinginezo wauze kwa bei hiyo wapate faida.