RC Makonda amsifu Meya wa Chadema

Muktasari:

Makonda alitoa kauli ya kumsifia meya huyo katika sherehe za uzinduzi wa wiki ya maji

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Paul Makonda amesifia utendaji kazi wa meya wa jiji Isaya Mwita kwa kile alichodai hayumbishwi na misimamo ya vyama.

Akizungumza leo Machi 16, Makonda alisema Mwita ambaye ni diwani wa Chadema hana tabia kama za wenzake na muda mwingi anafikiria maendeleo.

Akiwa katika uzinduzi wa wiki ya maji baada ya Mwita kumkaribisha kuzungumza, Makonda alianza kwa kumtania,

"Meya nilijua utazungumzia maandamano ila niseme wazi namkubali sana Isaya, ni miongoni mwa watu ambao unaweza kukaa nao mkazungumzia maendeleo."

"Hii ndiyo aina ya maandamano inayotakiwa. Tunataka kuandamana kwa kujadili na kutafuta ufumbuzi wa changamoto kwa wananchi tunaowaongoza.

"Wangekuwa wale wengine wangejiweka huko lakini huyu anapenda maendeleo.

"Wengine wanasubiri wawaingize watoto wa watu barabarani waandamane wavunjwe miguu halafu wawatafute watu wa Ulaya wawape hela," amesema Makonda.