Msanii Baba Levo apandishwa kizimbani

Muktasari:

Kafikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma akikabiliwa na mashtaka matatu


Kigoma. Diwani wa Mwanga Kaskazini  (ACT-Wazalendo) Manispaa ya Kigoma Ujiji, Clayton Chipando maarufu Baba Levo amepandishwa kizimbani leo Ijumaa Mei 4, 2018 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kigoma akikabiliwa na mashtaka matatu.

Wakili wa Serikali, Antia Julius amesema mshtakiwa huyo alitenda makosa hayo April 12, 2018 katika Zahanati ya Msufini iliyopo Kata ya Mwanga Kaskazini.

Amesema mshtakiwa huyo ambaye pia ni msanii wa muziki wa kizazi kipya anakabiliwa na mashtaka ya kutoa lugha ya matusi, shambulio la kudhuru mwili na kufanya fujo katika zahanati hiyo, akidaiwa kumpiga muuguzi, Christina Gervas.

Antia amesema Clayton amefunguliwa kesi namba 62/ 2018 na anashitakiwa kwa mujibu wa kifungu cha 89 (1) (a) ya kanuni ya adhabu.

Hakimu mkazi mfawidhi wa Mahakama hiyo, Frola Mtarania alimueleza Baba Levo kuwa dhamana yake ipo wazi  kutokana na shitaka linaomkabili, ambao mshtakiwa huyo alifanikiwa kupata wadhamini wawili na yupo nje kwa dhamana.