Magaidi waua 14 kanisani Burkina Faso

Muktasari:

  • Walitumia pikipiki na kuvamia waumini waliokuwa wakifanya ibada kanisani kisha kuwafyatulia risasi.

Burkina Faso. Watu wanaodhaniwa ni magaidi wameshambulia kanisa moja nchini Bukina Faso na kuua 14.

Tukio hilo limetokea jana Jumapili Desemba Mosi wakati waumini wa Kanisa la Hantoukoura lililopo Mashariki mwa nchi hiyo wakihudhuria ibada.

Watu walioshuhudia tukio hilo walisema, waliwaona watu wenye silaha wakiingia katika kanisa hilo na kuanza kufyatua risasi ovyo na kujeruhi kadhaa.

Taarifa ya Jeshi la Polisi nchi humo ilihusisha tukio hilo kufanywa na kundi la kigaidi la Jihadist.

Shirika la habari la Ufaransa (AFP), lilisema kuwa watu hao wanaume walitumia pikipiki waliteketeza waumini kadhaa wakiwamo wachungaji na watoto.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kundi hilo limehusika katika matukio kadhaa ya kihalifu na kuua mamia ya wananchi kwa miaka mingi.

“Sababu kubwa ni mvutano wa kikabila na kidini haswa katika mpaka wa Mali,” ilisisitiza taarifa hiyo.

Matukio ya kigaidi yameongezeka nchini Burkina Faso tangu mwaka 2015 na kusababisha maelfu ya shule kufungwa ambako Oktoba mwaka huu, 15 waliuawa na wengine wawili kujeruhiwa katika shambulio lililotokea katika msikiti.