17,000 wamejipima wenyewe VVU nchini Tanzania

Muktasari:

Watu zaidi ya 17,000  wamejipima wenyewe maambukizi ya Virusi vya Ukimwi (VVU) kwa kutumia vifaa maalumu vilivyozinduliwa hivi karibuni.

Mwanza. Watu zaidi ya 17,000  wamejipima wenyewe maambukizi ya Virusi vya Ukimwi (VVU) kwa kutumia vifaa maalumu vilivyozinduliwa hivi karibuni.

Hayo yameelezwa leo Jumapili Desemba Mosi, 2019 na Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu, “wamejipima wakati wa majaribio na utafiti wa matumizi na ufanisi wa mashine hizo.”

Akizungumza wakati wa kilele cha maadhimisho ya siku ya Ukimwi duniani, Waziri Ummy amesema hao ni kati ya zaidi ya watu 27,000 waliopewa mashine hizo wakati wa majaribio.

"Kuna maneno kuwa watu wakijipima wenyewe na kugundua wameathirika wanaweza kujiua au kwenda kuambukiza wengine makusudi. Naomba niwatoe hofu wananchi kuwa madai hayo sio sahihi.”

"Kati ya watu 26,000 waliopokea mashine za kujipima wenyewe wamepima na kurejesha majibu wenyewe,” amesema Ummy.

Amesema pamoja na kutunga sheria kuruhusu watu kujipima wenyewe VVU, Serikali ya Tanzania pia imeruhusu watoto wenye umri chini ya miaka 18 kupima virusi bila kulazimika kupata kibali cha mzazi au mlezi.