Dk Tulia awakatia bima ya afya wazee 3420 mkoani Mbeya

Muktasari:

Taasisi ya Tulia Trust (TT) amezindua mpango wa kuwasaidia wazee na wanaoishi katika mazingira magumu mjini Mbeya kwa kuwalipia fedha kwenye Mfuko wa Afya ya Jamii Ulioboreshwa (ICHF).

Mbeya. Taasisi ya Tulia Trust (TT) amezindua mpango wa kuwasaidia wazee na wanaoishi katika mazingira magumu mjini Mbeya kwa kuwalipia fedha kwenye Mfuko wa Afya ya Jamii Ulioboreshwa (ICHF).

Hadi leo Jumapili Januari 19, 2020 Tulia Trust ambayo mkurugenzi wake ni naibu Spika wa Bunge la Tanzania, Dk Tulia Ackson imewakatia bima ya afya watu 3,420 ambao ni wazee na wanaoishi katika mazingira magumu kutoka kaya 570.

Jackline Boaz, meneja wa Tulia Trust amesema mpango huo ulianzishwa mwaka 2019 na Dk Tulia, “ leo ndio tunazindua rasmi mpango huu lakini wazee hawa walianza mwaka jana kunufaika na bima ya afya.”

“Lengo la Tulia Trust ni kuona wazee na wanaoishi kwenye mazingira magumu wanakuwa na uhakika wa matibabu. Tutaendelea kusaidia kwenye suala la afya kikamilifu.”

Amesema wanawatambua wenye uhitaji kupitia kwa viongozi wa Serikali za mitaa na kata wa Jiji la Mbeya.