Magufuli ateua wenyeviti bodi ya Latra, TFRA

Muktasari:

Taarifa iliyotolewa leo Jumatano Septemba 11, 2019 na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu imesema Rais John Magufuli ameteua wenyeviti wawili wa Bodi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Ardhini (Latra) na Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA).

Dar es Salaam. Rais wa Tanzania, John Magufuli amemteua Dk John Ndunguru kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Ardhini (Latra).

Taarifa iliyotolewa leo Jumatano Septemba 11, 2019 na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais Ikulu imemnukuu Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi ikisema uteuzi wa Dk Ndunguru umeanza Septemba 9, 2019.

Pia, taarifa hiyo imesema Rais Magufuli amemteua Profesa Antony Mshandete kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA).

Profesa Mshandete ni Naibu Makamu Mkuu wa Chuo (Taaluma, Utafiti na Ubunifu), Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) kilichopo mkoani Arusha.

Imesema uteuzi huo umeanza Septemba 9, 2019.