Makonda ataka usafi Dar kuendelea kama ilivyokuwa katika mkutano Sadc

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam nchini Tanzania, Paul Makonda 

Muktasari:

Katika mkutano wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (Sadc) uliomalizika Agosti 18, 2019 usafi hasa katikati ya Jiji la Dar es Salaam ulikuwa wa hali ya juu, sasa mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda anataka usafi huo kuendelea siku zote.


Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam nchini Tanzania, Paul Makonda amewataka wakazi wa mkoani humo kuweka mazingira yao safi kama walivyofanya wakati wote wa mkutano wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (Sadc) uliomalizika Agosti 18, 2019.

Mkutano huo uliohusisha wakuu wa nchi 16 huku ikishuhudiwa Rais wa Tanzania, John Magufuli akichaguliwa kuwa mwenyekiti wa jumuiya hiyo.

Makonda amewataka wananchi kuweka mazingira yao katika hali ya usafi, wasisubiri kusukumwa kufanya hivyo.

“Niwashukuru wananchi wa Mkoa huu wameonyesha ushirikiano mzuri katika kipindi hiki cha mkutano wa Sadc. Tuendeleze usafi sio tena  wageni wanarudi wanakuta mazingira yamebadilika tutaaibika,” amesema Makonda.

Amevishukuru vyombo vya ulinzi na usalama na wananchi kwa kudumisha amani na usalama.