Mangula: CCM itafuta upinzani uchaguzi mkuu 2020

Muktasari:

Makamu mwenyekiti wa CCM-Bara, Philip Mangula amesema chama hicho tawala nchini Tanzania kitashinda viti vyote vya udiwani, ubunge na urais katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 2020 na kuvifuta vyama vya upinzani.

Sengerema. Makamu mwenyekiti wa CCM-Bara, Philip Mangula amesema chama hicho tawala nchini Tanzania kitashinda viti vyote vya udiwani, ubunge na urais katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 2020 na kuvifuta vyama vya upinzani.

Ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Februari 14, 2020 wilayani Sengerema Mkoa wa Mwanza alipokutana na viongozi wa ngazi mbalimbali wilayani Sengerema.

Amesema mwaka 2020 ni wa uchaguzi, CCM lazima ihakikishe inashinda, kuwataka viongozi kufanikisha jambo hilo kwa kuteua wagombea sahihi ili kuepusha malumbano.

"Tunapaswa kushirikiana wote kuanzia ngazi za mashina hadi Taifa,  tukifanya hivyo tutashinda kwa nguvu moja,” amesema Mangula akisisitiza kuwa  siasa safi na ushirikiano na Serikali ni msingi wa maendeleo.

Katibu wa CCM Mkoa wa Mwanza, Salum Kaly amemhakikishia Mangula kuwa Mkoa huo kutekeleza yote waliyoelezwa.