Mashahidi 28 kumkabili ayeedaiwa kumuua mkewe

Muktasari:

Mfanyabiashara Hamisi Luongo (38) anadaiwa kumuua mke wake, Naomi Marijani kisha kumchoma moto kwa kutumia magunia mawili ya mkaa

Dar es Salaam. Mashahidi 28 na vielelezo sita, vinatarajia kutolewa katika kesi ya mauaji inayomkabili, mfanyabiashara Hamisi Luongo (38).

Luongo anakabiliwa na shtaka moja la kuua mke wake Naomi Marijani, kisha kumchoma moto kwa kutumia magunia mawili ya mkaa na baadaye kuchukua majivu yake na kwenda kuzika  shambani kwake eneo la Vikindu, wilayani Mkuranga.

Umuazi huo umetolewa leo Jumatano, Oktoba 21, 2020 na Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Kisutu, Huruma Shaidi wakati kesi hiyo ilipoitwa kwa ajili ya mshtakiwa kusomewa maelezo yake.

Hatua hiyo imefikiwa baada ya Mahakama Kuu kutoa  kibali kwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kukaa kama Mahakama Kuu na kusikiliza kesi ya mauaji.