Matokeo mazuri darasa la saba Dar neema kwa walimu

Muktasari:

  • Baada ya Mkoa wa  Dar es Salaam kushika namba moja kwa kupata ufaulu wa asilimia 93.28 katika matokeo ya kumaliza elimu ya msingi mwaka 2019, walimu mkoani humo watapewa tuzo maalumu.

Dar es Salaam. Baada ya Mkoa wa  Dar es Salaam kushika namba moja kwa kupata ufaulu wa asilimia 93.28 katika matokeo ya kumaliza elimu ya msingi mwaka 2019, walimu mkoani humo watapewa tuzo maalumu.

Hayo yameelezwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, kubainisha kuwa hilo linatokeana na jitihada zilizofanywa na walimu wa Mkoa huo kufikia mafanikio hayo, wana kila sababu ya kupewa tuzo.

Mikoa mingine iliyofanya vizuri ni Arusha, Iringa, Kagera, Katavi, Kilimanjaro, Mbeya, Simiyu, Njombe na Pwani huku ufaulu kwa ngazi ya halmashauri, jiji la Arusha likiongoza na kufuatiwa na Ilemela, Kinondoni, Mwanza jiji, Ilala Manispaa, Moshi Manispaa, Bukoba Manispaa, Iringa Manispaa, Biharamulo na Arusha.

Makonda amesema kabla mwaka 2019 kumalizika, atawafanyia sherehe na kuwapatia tuzo na zawadi walimu waliofanya vizuri zaidi kama ambavyo amekuwa akifanya kwa askari wa jeshi la polisi.

“Walimu wamefanya kazi kubwa na matokeo yake tunayaona  kwa miaka mitatu  mfululizo mkoa wa Dar tunafanya vizuri, wanastahili zawadi.”

“Kuongoza darasa la saba inatupa taswira ya kuongoza kidato cha nne na hata cha sita, Mkoa wetu una uwezo huo na hata hiyo mikoa mingine inayoongoza kwa ngazi zinazofuatia, ukifuatilia hao wanafunzi wametoka Dar es Salaam,” amesema Makonda.

Makonda amesema pia atatoa zawadi kwa wahudumu wa sekta ya afya waliofanya vizuri katika kutoa huduma bora kwa wananchi mwaka 2019.

“Watoa huduma za afya wanafanya kazi kubwa kila siku,  wanawake wanajifungua salama, wagonjwa wanahudumiwa na wanafanya kazi bila kuchoka tuna kila sababu ya kuwapongeza,” amesema Makonda.