VIDEO: Mfumuko wa bei Tanzania waongezeka

Kaimu Mkurugenzi wa Sensa ya Watu na Jamii wa ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Ruth Minja

Muktasari:

Mfumuko wa bei nchini Tanzania KWA mwezi Novemba 2019 umeongezeka hadi asilimia 3.8 kutoka asilimia 3.6 ya mwezi Oktoba, 2019.

Dodoma. Mfumuko wa bei nchini Tanzania Kwa mwezi Novemba 2019 umeongezeka hadi asilimia 3.8 kutoka asilimia 3.6 ya mwezi Oktoba, 2019.

Kaimu Mkurugenzi wa Sensa ya Watu na Jamii wa ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS), Ruth Minja ameyasema hayo leo Jumanne Desemba 10, 2019 mjini Dodoma.

Amesema hali hiyo inaashiria kuongezeka kwa kasi ya mabadiliko ya bei ya bidhaa na huduma kwa mwezi Novemba 2019.

"Kuongeza kwa mfumuko wa bei kumechangia  na kuongeza kwa bei za baadhi ya bidhaa  za vyakula na bidhaa zisizo za vyakula kwa kipindi kilichoishia  Novemba  2019, "amesema.

Ametaja baadhi ya vyakula vilivyoongezeka bei kuwa ni mchele kwa asilimia 6.6, unga wa mihogo (7.8), nyama (2.6), mafuta ya kupikia (7.2), maharage (8.6), mbogamboga (6.0) na mihogo kwa asilimia 5.8.

Kwa upande wa bidhaa zisizo za vyakula zilizoongezeka bei kwa mwezi Novemba 2019 ni pamoja na mavazi kwa asilimia 2.7, mkaa (4.4), samani (3.1), huduma ya malazi kwa wageni (5.0) na mazulia kwa asilimia 6.3.