RAS Morogoro azungumzia ujenzi wa mnala, uzio makaburi ya ajali ya lori

Muktasari:

Ujenzi wa uzio katika makaburi ya Kolla walipozikwa marehemu wa ajali ya lori la mafuta ya petroli lililoanguka kisha kulipuka moto mkoani Morogoro haujaanza.


Morogoro. Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Morogoro (RAS), Noel Kazimoto amesema suala la ujenzi wa uzio na mnara katika makaburi ya Kolla walikozikwa marehemu wa ajali ya lori la mafuta ya petroli.

Lori hilo liliangusha kisha kulipuka Jumamosi ya Agosti 10,2019  eneo la Msamvu mkoani Morogoro ambapo hadi leo Jumatatu mchana, idadi ya vifo vimefikia 97 huku majeruhi 18 wakiwa chumba cha uangalizi maalum (ICU) cha Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) jijini Dar es Salaam.

Pia, majeruhi 16 wamelazwa Hospitali ya Rufaa ya Morogoro kwa matibabu zaidi.

Akizungumza na Mwananchi leo Jumatatu, Kazimoto kwa niaba ya Mkuu wa mkoa huo, Dk Stephen Kebwe amesema kamati ya maafa imekutana na kujadili mambo mbalimbali likiwemo la uzio na mnara.

Amesema makubaliano yameonelea kukutana na wadau ili kuona namna ya kuchangia na kuanza kwa ujenzi.

"Tukishakutana na wadau na kujadiliana nao namna ya kuchangia ujenzi kuanza, tunatarajia kukutana nao kati ya Agosti 21 au 22 na baada ya hapo ujenzi utaanza," amesema Kazimoto

Aidha amesema mbali na kujengwa kwa uzio huo, kila kaburi litawekewa alama ya kudumu tofauti na zilizopo sasa za mbao ambazo zinaweza kuliwa na mchwa.