Sakata la askari aliyeokotwa mtaroni, mke asimulia alivyoagana naye

Hai. Mke wa askari wa upelelezi wa kituo cha polisi Kia, Asnati Yango amezungumzia namna alivyoagana na mume wake kabla hajaokotwa kwenye mtaro akiwa amefariki dunia.

Mwili wa Juma Yango (59) uliokotwa kwenye mtaro juzi ukiwa na jeraha kubwa kisogoni, jirani na mgahawa wa chakula bora mita chache kutoka kituo cha polisi wilayani hai Mkoa wa Kilimanjaro.

Akizungumza jana nyumbani kwake, Asnati alisema mume wake alikuwa nyumbani na alikula chakula cha mchana na kumuaga kuwa anakwenda kazini na kwamba alikuwa na zamu ya usiku.

Alisema siku ya Pasaka mume wake alikuja nyumbani mchana wa saa sita na kushiriki chakula cha mchana na baadaye kuaga kuwa anakwenda kazini.

“Aliondoka saa kumi jioni na kuaga kuwa anakwenda kazini kama kawaida yake na sikuwasiliana naye tena hadi hapo jana saa nne asubuhi nilipopewa taarifa kuwa ameokotwa mtaroni akiwa amekufa,” alisema Asnati.