Sugu: Hata bila tume huru ya uchaguzi Chadema inashinda Mbeya

Muktasari:

Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi maarufu Sugu amesema atagombea ubunge katika uchaguzi mkuu wa Oktoba, 2020 na ana uhakika ataibuka mshindi.

Mbeya. Mbunge wa Mbeya Mjini (Chadema), Joseph Mbilinyi maarufu Sugu amesema atagombea ubunge katika uchaguzi mkuu wa Oktoba, 2020 na ana uhakika ataibuka mshindi.

Sugu ameeleza hayo leo Jumatano Februari 26, 2020 katika mkutano wa chama chake na waandishi wa habari jijini Mbeya.

"Kuna watu wanauliza kama nitagombea nataka niwaambie ntagombea siyo kugombea tu nitashinda. Kuwe na tume huru (ya uchaguzi) au isiwepo Chadema lazima ishinde Jiji la Mbeya kwa sababu tutahakikisha kura zinapigwa na tunazilinda,” amesema Sugu.

Amesema Chadema kimeandikisha wanachama hai 68,000 hadi Oktoba, 2020 wana uhakika wa kuandikisha wanachama zaidi ya 100,000, akisisitiza kuwa idadi hiyo ni kura za uhakika.

Jana  katika mazungumzo yake ya Mwananchi mbunge huyo alimtumia salamu katibu mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally akibainisha kuwa madiwani 11 wa Chadema katika Jiji la Mbeya kuhamia chama tawala hakuwezi kubadili mapenzi ya wananchi wa Mbeya kwa Chadema.

Alieleza hayo ikiwa ni siku moja baada ya madiwani hao, akiwemo Meya wa Jiji la Mbeya, Mchungaji David Mwashilindi kujivua nyadhifa zao na kuhamia CCM.

Madiwani hao walipokelewa juzi Jumatatu na Dk Bashiru katika ofisi za makao makuu ya CCM jijini Dodoma huku mtendaji mkuu huyo wa CCM akisema hizo ni salamu kwa Sugu kuelekea uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba, 2020.

Madiwani hao  na kata zao kwenye mabano ni Mwashilindi (Nzovwa), naibu Meya, Fanuel Kyanula (Sinde); Fabian Sanga (Ghana); Anyandwile Mwalwiba (Isanga);  Dickson Makilasa (Ilomba); Constantine Mwakyoma (Kalobe); Furaha Mwandalima (Ilomi); Anderson Ngao (Mwasanga); Ibrahim Mwampwani (Isyesye); Henry Mwangambaku (Forest) na Kigenda Kasebwa (Viti Maalumu).

“Dk Bashiru mwenyewe Mbeya haijui, ameuziwa mbuzi kwenye gunia, amechukua watu ambao hawana ‘future’ kwenye maeneo yao na wala wasingepita kwenye kura za maoni.”

“Unachoweza kujiuliza kwa nini Bashiru  haongezi wapiga kura lakini  anahangaika kutafuta wanaopigiwa kura?” amehoji Sugu.

Sugu amesema madiwani hao kuondoka Chadema kumezidisha hasira kwa wakazi wa Mbeya, “ambao sasa wameongezeka kujiandikisha, yaani mimi sasa hivi malengo ni kufikia Juni niwe nimesajili wananchi 100,000. Yeye muache ahangaike na wapigiwa kura badala ya wapiga kura.”

Amesema licha ya madiwani hao kuondoka, bado wana idadi kubwa ya madiwani hivyo wataendelea kuongoza Jiji hilo.

“Suala la ubunge na kura za urais Mbeya tulikwisha kulimaliza tangu mwaka 2010, wakiwa hawaamini basi wasubiri wataona,” amesisitiza.

Amesema Dk Bashiru anatakiwa kujikita zaidi kumshauri mwenyekiti wa CCM, Rais John Magufuli ili  atekeleze ahadi alizowaahidi wananchi katika kampeni za mwaka 2015, ikiwa ni pamoja na ujenzi wa barabara ya  Mapelele kata ya Ileni jimbo la Mbeya Mjini. Amesema barabara hiyo haijajengwa licha ya ahadi kutolewa mwaka 2015.