Hezbollah yarusha makombora Israel kulipiza kisasi

Muktasari:

  • Siku moja baada ya kiongozi wa kundi la Hezbollah kusema watalipiza kisasi Israel kutokana na mauaji ya Naibu Kiongozi wa Hamas, jana Jumamosi kundi hilo limedai kurusha makombora zaidi ya 60 kaskazini mwa Israel.

Lebanon. Kundi la wanamgambo la Hezbollah la nchini Lebanon limesema limerusha makombora zaidi ya 60 nchini Israel ikiwa ni hatua ya kwanza ya kulipiza kisasi kwa nchi hiyo.

Makombora hayo yamerushwa jana Jumamosi, Januari 6, 2023 katika kambi ya kijeshi ya Israel kujibu mauaji yaliyotokea Beirut ya Naibu Kiongozi wa wanamgambo wa Hamas, Sahel al-Arouri kutoka Palestina.

AFP imesema jana ving'ora vya mashambulizi ya anga vilisikika katika miji ya kaskazini mwa Israel na katika miinuko ya milima Golan.

Mpaka kati ya Israel na Lebanon kumekuwa na kurushiana risasi karibu kila siku tangu vita vya Israel na Hamas vilipozuka Oktoba 7, mwaka jana.

Mauaji ya Arouri yaliyotokea Jumanne kwenye ngome ya Hezbollah kusini mwa Beirut, yamezidisha hofu ya mapigano zaidi.

Kiongozi wa Hezbollah alisema atalipiza kisasi na hawaiogopi Israel, huku jeshi la Israel nalo likiweka bayana kuwa yeye ndiye lengo lao kwa sasa.

Katika hotuba yake ya mwisho wa juma, kiongozi huyo Hassan Nasrallah aliionya Israel kwamba kundi hilo litajibu haraka mauaji ya Arouri.

Kwa upande wa Jeshi la Israel limesema limekiri makombora hayo kutoka ardhi ya Lebanon lakini halijasema chochote kuhusu mashambulizi dhidi ya kambi yake ya jeshi.