Seneta atimuliwa bungeni kwa kuvaa suti ya madoa ya hedhi
Seneta wa Kenya, Gloria Orwoba
Nairobi. Seneta wa Kenya, Gloria Orwoba amefukuzwa bungeni baada ya kuhudhuria vikao baada ya kuvalia suti nyeupe iliyokuwa na alama rangi nyekundu (kuashiria hedhi) ikiwa ni moja ya kampeni yake ya kushinikiza upatikanani wa taulo za hedhi kwa wasichana bure.
Orwoba ambaye ni kutoka muungano unaotawala, anatarajiwa kuwasilisha hoja kuhusu muswada wa kutoa taulo za bure leo Jumatano Februari 15 ikiwa ni sehemu ya juhudi zake za kumaliza tatizo hilo kwa watoto wa kike nchini humo.
Maseneta wa Kenya walilazimika kukatiza kikao jana Jumanne Februari 14 alasiri ili kumfahamisha spika kwamba Owoba alikuwa amevaa mavazi yanayoashiria jambo, japo yalikuwa kinyume na mavazi yenye staha kwa mwonekano wa maseneta bungeni.
Akionyesha kutoridhishwa na agizo la Spika, Seneta huyo aliisema: "Nashangaa kwamba mtu anaweza kusimama hapa na kusema kwamba bunge limefedheheshwa kwa sababu mwanamke amepata hedhi."
Spika Amason Kingi aliamuru seneta huyo kwenda kubadilisha nguo zake ndipo ataruhusiwa bungeni, jambo ambalo lilifanyika baada ya kutii agizo hilo.
“Siyo kosa kuwa na hedhi... Seneta Gloria nasikitika unapitia hali ya kimaumbile, suti yako imepata madoa ya ajabu, naomba uondoke ili ukabadilishe urudi na nguo ambazo hazina madoa," amesema.
Muda mfupi baada ya kutoka nje ya ukumbi Seneta Owoba alizungumza na waandishi wa habari, amesema lengo lake ni kutokomeza tatizo linalotokana na unyanyapaa wa hedhi.
“Baadhi ya mambo ambayo ninayotetea na kutunga sheria na kuhakikisha kwamba kutolewa bure taulo za hedhi kwa watoto wote wanaokwenda shule," amesema Orwoba.
Seneta huyo aliwasili bungeni akiwa amevalia suti nyeupe ikiwa na doa jekundu katikati ya miguu.