Viongozi 18 wa nchi akiwemo Rais Samia kumuaga Geingob
Muktasari:
- Leo, Februari 24, 2024, yanafanyika mazishi ya kitaifa ya aliyekuwa Rais wa Namibia, Hage Geingob aliyefariki dunia Februari 4, 2024. Wakuu wa nchi na Serikali wanatarajia kutoa heshima zao za mwisho kwa kiongozi huyo.
Windhoek. Viongozi 18 wa mataifa mbalimbali watashiriki shughuli ya kumuaga aliyekuwa Rais wa Namibia, Hage Geingob katika mazishi ya kitaifa yanayofanyika leo, Februari 24, 2024 mjini Windhoek.
Wengi wa viongozi hao ni kutoka nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) akiwemo Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ambaye ameshawasili nchini humo kwa ajili ya kutoa heshima za mwisho.
Geingob (82), alifariki dunia Februari 4, 2024 katika hospitali moja nchini humo wakati akipatiwa matibabu ya saratani yanayotajwa kuwa chanzo cha kifo chake.
Kiongozi huyo aliyeshiriki harakati za kupigania ukombozi wa nchi hiyo kupitia chama cha Swapo, atazikwa kesho, Februari 25, 2024 katika makaburi maalumu ya viongozi nchini humo, maarufu kama Heroes Acres".
Mwili wa Geingob umewekwa katika viwanja vya Bunge la nchi hiyo tangu jana, Februari 23, 2024 kwa ajili ya wananchi kutoa heshima za mwisho na shughuli hiyo inatarajiwa kumalizika leo, saa 5 asubuhi, kabla ya kuanza kwa ibada ya mazishi ya kitaifa na wakuu wa nchi kupata nafasi ya kumuaga.
Rais wa Namibia, Nangolo Mbumba atawaongoza wakuu wa nchi pamoja na wawakilishi wa mataifa mengine katika shughuli hiyo inayotarajiwa kuhudhuriwa na mamia ya wananchi wa Namibia na mataifa jirani.
Geingob aliyekuwa Rais wa Namibia tangu mwaka 2014, alitarajiwa kumalizia muda wake Novemba 2024, na tayari chama chake cha Swapo kilikuwa kimemchagua Netumbo Nandi-Ndaitwah kuwa mgombea urais kwenye uchaguzi mkuu ujao.
Kwa mujibu wa Katiba ya Namibia, Rais anapofariki, makamu wake ndiyo anachukua madaraka. Hivyo, Nangolo Mbumba aliapishwa kuwa Rais wa nchi hiyo muda mfupi baada ya kifo cha Geingob, naye akamteua Nandi-Ndaitwah kuwa makamu wake.
Mbumba ameahidi kulivusha Taifa hilo kwenye kipindi hiki cha mpito kuelekea kwenye uchaguzi ujao na amesisitiza hatagombea kwenye uchaguzi huo unaotarajiwa kufanyika Novemba 2024.
Geingob aliyezaliwa kaskazini mwa Namibia mwaka 1941, alikuwa Rais wa kwanza wa Namibia kutoka nje ya kabila la Ovambo ambalo ni zaidi ya nusu ya watu katika nchi hiyo.
Alianza harakati dhidi ya utawala wa kibaguzi wa Afrika Kusini ambayo wakati huo ilitawala Namibia, tangu miaka yake ya awali ya shule kabla ya kufukuzwa uhamishoni.
Alikaa karibu miongo mitatu nchini Botswana na Marekani, ukiacha ile ya zamani kwa muongo wa pili mwaka 1964.
Kiongozi huyo alisoma katika Chuo Kikuu cha Fordham huko New York, Marekani na baadaye alipokea Shahada ya Uzamivu (PhD) nchini Uingereza.
Akiwa Marekani, aliendelea kuwa mtetezi mkubwa wa uhuru wa Namibia, akiwakilisha vuguvugu la ukombozi wa ndani (Swapo), ambacho sasa ni chama tawala, katika Umoja wa Mataifa na kote Marekani.
Mapema miaka ya 1970, alianza kazi katika Umoja wa Mataifa katika idara ihusuyo masuala ya utawala.
Akionekana kama kiongozi mkuu, alirejea Namibia mwaka 1989, mwaka mmoja kabla ya uhuru wa nchi hiyo.
“Nilikumbatia ardhi ya Namibia baada ya miaka 27 uhamishoni. Nikikumbuka nyuma, safari ya kujenga Namibia mpya imekuwa ya manufaa,” alisema katika ukurasa wake wa X (Twitter) mwaka 2020 akiweka picha ya mdogo wake akibusu lami baada ya kutua nyumbani.
Swapo iliposhinda uchaguzi wa kwanza mwaka wa 1990, Geingob aliteuliwa kuwa Waziri Mkuu, nafasi aliyoshikilia kwa miaka 12 kabla ya kurejea tena mwaka 2012.
Mwaka 2014, chama kiliposhinda uchaguzi mwingine, kikizingatia urithi wa jukumu lake katika mapambano ya ukombozi, Geingob akawa Rais.